Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia,Pwani

WAZIRI wa ardhi, Jerry Silaa amewahakikishia wakazi wa Mbala,Pingo -Chamakweza Chalinze mkoani Pwani kuwa atapeleka timu ya watalaamu wa ardhi ili kufanya uhakiki wa mipaka katika mgogoro uliodumu kwa miaka 25 ambao bado haujapata suluhu.

Aidha ametoa wito kwa mkoa
wa Pwani, kusimamia Halmashauri zake kupima na kupanga maeneo ili kuondoa changamoto ya migogoro ya ardhi ambayo inaweza kujitokeza.

Akizungumza katika ziara yake ya siku tatu aliyoianza Mbala, Chalinze mkoani Pwani ,Silaa alielezea timu hiyo itafanya kazi kwa kushirikisha wananchi kisha itamkabidhi taarifa sahihi ya uhakiki sanjali na utambuzi wa historia ya kijiji cha Chamakweza .

“Kazi hii ikimalizika itaenda sambamba na kutengeneza mpango wa matumizi bora ya ardhi”

Vilevile alitoa rai kwa wakulima na wafugaji wa eneo la Mbala,Chamakweza kuendeleza amani na upendo hadi hapo mgogoro huo utakapokamilika.

“Nchi hii inaendeshwa kwa sheria, nilichogundua hapa kuna sintofahamu halisi ama ya kutengeneza, kiserikali lazima kuna taarifa ya kujua kijiji hiki kimeanza lini, mwaka gani,kujua hii Chamakweza ilianza lini”

Silaa alielezea ,sheria namba 5 ya ardhi inatoa mamlaka ya ardhi kwenye mkutano Mkuu wa kijiji,nje ya hapo ni uvunjifu wa sheria.

Waziri huyo akiwa Kikongo alieleza, suluhu ya migogoro mingi ya ardhi ni kufanya opereshen za mara kwa mara pamoja na watu kuheshimu ardhi zinazomilikiwa kihalali pasipo kuvamia.

Silaa anasema, kwasasa kutakuwa na ofisi ya Kamishna wa ardhi mkoani Pwani katika mgawanyo wa pande mbili,ili kusogeza huduma ya kupunguza migogoro ya ardhi.

Awali Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge,aliagiza kusiwepo na shughuli ya uuzaji maeneo katika kijiji hicho hadi hapo mgogoro utakapotatuliwa.

Kunenge alisema Hakuna aliyejuu ya sheria, na ambae yeyote atabainika kusababisha uvunjifu wa amani atachukuliwa hatua kali na kukamatwa.

Akitoa picha ya migogoro mikubwa ,alisema ni pamoja na ile ya kata ya Mapinga lakini anamshukuru Waziri kwa kulitendea haki eneo hilo.

Kunenge anasema, walikuwa na kampeni ya Tokomeza migogoro ya ardhi Pwani ambayo imesadia kwa kiasi kikubwa kupunguza migogoro ya ardhi kwa kuifanyia maamuzi.