▪️Awataka wenye leseni kufuata taratibu za kisheria za msaada wa kiufund

▪️Serikali kutunga kanuni za kuratibu wageni kwenye Leseni ndogo

▪️Awataka RMO kufanya ukaguzi katika maeneo yao

▪️Awaonya wachimbaji wanaoingiza wageni kinyemela

📍Morogoro

Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amepiga marufuku raia wa kigeni kuingia na kufanya shughuli kwenye leseni za uchimbaji mdogo; hii ni kufuatia changamoto zilizobainika katika uingiaji mikataba ya utoaji wa misaada ya kiufundi kati ya wamiliki wa leseni ndogo za uchimbaji madini na raia wa kigeni.

Amesema hayo leo Februari 17, 2025 wakati akifungua Kikao Kazi cha kupokea maoni kutoka kwa wadau kuhusu mapendekezo ya kuandaa Rasimu ya Kanuni za Madini za Utoaji Msaada wa Kiufundi kwa Wamiliki wa Leseni Ndogo za Uchimbaji Madini za Mwaka 2025 kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Edema Hoteli Mkoani Morogoro.

Aidha, Waziri Mavunde ametoa wito kwa washiriki wote wa Kikao Kazi hicho kutoa maoni yao kwa uhuru na uwazi ili kusaidia upatikanaji wa Kanuni nzuri na inayotekelezeka kwa lengo la kuongeza tija katika mnyororo mzima wa shughuli za Sekta ya Madini nchini na kutekeleza sharti la kifungu cha 8(3) cha Sheria ya Madini Sura Namba 123.

“Katika kipindi cha muda mfupi tumeshuhudia mabadiliko makubwa kwenye Sekta ya Madini kutokana na utashi wa Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye anatamani kuona wachimbaji wadogo wanafikiwa, ambapo leo naagiza ofisi ya Kamishna kuwasaidia wachimbaji wadogo ili waweze kuhitimu kutoka hapo walipo na kuendelea mbele”

“Haiingii akilini, mgeni anakuja, anaingia kwenye leseni ya mchimbaji mdogo kupitia mkataba wa utoaji msaada wa kiufundi, wachimbaji wadogo hawanufaiki wala kuendelea zaidi kimatumizi ya teknolojia na mitaji, hili halikuwa lengo la Sheria katika kuweka sharti hilo ili kuendeleza wachimbaji wadogo”, alibainisha Waziri Mavunde.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Mavunde ametoa onyo kwa wachimbaji wadogo kutowakaribisha wageni bila kufuata utaratibu katika leseni za uchimbaji mdogo wa madini ambapo itapelekea kufutiwa leseni kwa atakaye kiuka agizo hilo na kutoa angalizo kwa Maafisa Madini Nchini kudhibiti uingiaji wa wageni bila kufuata taratibu.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema Kikao hicho kimelenga kupokea mapendekezo ya wadau kwa ajili ya kuandaa rasimu ya Kanuni za Msaada wa Kiufundi kwa ajili ya wamiliki wa leseni za uchimbaji mdogo ambapo Wizara iko huru na tayari kupokea maoni ya kila mdau.

Naye, Rais wa Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini Tanzania John Bina amempongeza Waziri Mavunde kwa uamuzi wa kuwashirikisha wadau wa Sekta ya Madini wakiwemo wachimbaji wadogo ili kuandaa rasimu ya Kanuni hizo kuliko kujifungia na kuandaa Wizara pekee.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa Wachimbaji Wadogo kutoka mikoa yote nchini, vyama vya wachimbaji wadogo wanawake Tanzania na wafanyabiashara wa madini nchini.