Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Singida

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Ridhiwani Kikwete, ameipongeza Benki ya CRDB
kwa kuwa na mifumo bora ya usalama na afya ya wafanyakazi, wateja na jamii kwa ujumla mahala pa kazi.

Akizungumza katika kilele cha maonesho ya OSHA yaliyofanyika kitaifa mkoani Singida, Waziri Kikwete amesema: “Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inaamini kuwa usalama na afya mahali pa kazi ni haki ya msingi kwa kila mfanyakazi nchini, Benki ya CRDB imeonyesha mfano mzuri wa kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria ya Afya na Usalama Kazini ya mwaka 2003, nawapongeza sana, nampongeza pia Mkurugenzi Mtendaji wake ndugu yangu Abdulmajid Nsekela, hongereni sana Benki ya CRDB.”

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu)
Riziwani Kikwete (katikati) akipata maelezo mafupi kutoka kwa Meneja wa Afya na Usalama Kazini wa Benki ya CRDB, Salumu Shomali (wapili kulia) wakati alipotembelea banda la benki ya CRDB katika
maonesho ya OSHA yaliyofanyika kitaifa katika viwanja vya Mandewa mkoani Singida.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda, amesema Benki ya CRDB ni kati ya taasisi chache nchini zinazotekeleza kwa ufanisi kanuni za usalama kazini, na kusema ni taasisi bora inayoonyesha jinsi ya kuepuka majanga ya asili.

Meneja wa Afya na Usalama Kazini wa Benki ya CRDB, Salumu Shomali amesema: “Kila mwaka tunawafanyia uchunguzi wa afya wafanyakazi wetu uchunguzi wa afya wa kila mwaka na madaktari bingwa.”

Katika maonesho hayo, amesema zaidi ya watu 400 walipata vipimo vya afya, na baadhi yao walipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida kwa matibabu zaidi.

Katika maonesho hayo, Benki ya CRDB imeshinda tuzo ya mshindi wa tatu katika kipengele cha shughuli za fedha na bima katika kudumisha usalama wa wafanyakazi katika sekta ya fedha.