Na Cresensia Kapinga, JamhuriMedia, Namtumbo

Wananchi wa Kijiji cha Mtakanini kilichopo katika Kata ya Msindo Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma wameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuona umuhimu wa kusogeza huduma ya Madaktari bingwa kwa watu wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo, saratani ya kizazi na tezi dume kwenye vituo vya Alafya Wilayani humo.

Shukrani hizo zimetolewa mwishoni mwa wiki na wananchi wa kijiji cha Mtakanini wakiongozwa na Diwani wa Kata ya Msindo Remna Nchimbi wakati walipompokea Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Profesa Mohamedi Janabi ambaye alifika kwenye kituo cha Afya Mtakanini kuungana na Madaktari Bingwa 3 waliokuwa wakiendelea Kutoa huduma kwa wagonjwa kwa magojnwa ya Moyo,Kisukari,Tezi dume na kansa ya shingo ya kizazi kwa akina mama.

Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Vita Kawawa akimshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa Hospital ya Taifa ya Muhimbili Dkt. Mohamed Janabi mara baada ya kuwasili katika kituo cha Afya cha Mtakanini kilichopo kata ya Msindo Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma.

Nchimbi alisema kuwa kitendo cha Serikali kuwaleta madaktari bingwa toka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kimeleta matumaini makubwa kwa wananchi ambao wamekuwa wakisumbuliwa na magonjwa ambayo yanahitaji kuonana na madaktari bingwa kwa lengo la kupata tiba ambao wako mbali na maeneo ya vijiji.

Diwani Nchimbi aliiomba Serikali kupitia Wizara ya Afya iangalie uwezekano wa kuwa na mpango endelevu kwa madaktari bingwa ambao wako kwenye Hospitali za rufaa ikiwemo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kufika kila mara kwenye vituo vya Afya Kutoa huduma kwa wagonjwa kwa lengo la kupunguza changamoto zinazo wakabili za kufuata huduma hiyo kwenye Hospitali za rufaa au Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Vita Kawawa alisema kuwa amefurahishwa na kazi nzuri zilizofanywa na Madaktari Bingwa ambao walianza kazi hiyo ya kuwahudumia wangonjwa wa magonjwa ya Moyo,Kisukali,kansa ya shingo ya kizazi kwa wanawake na tezi dume katika Hospitali ya Serikali ya Wilaya ya Namtumbo na baadae walikwenda Kutoa huduma hiyo kwenye kituo cha Afya Lusewa pia walitoa huduma kwenye vituo vya Afya Mputa na Mtakanini jambo ambalo limeleta faraja kubwa sana kwa wananchi wa Wilaya ya Namtumbo kwani wengi wao walikuwa wakishindwa kupata tiba kutokana na gharama kubwa ya matibabu ambayo kwa kipindi cha zaidi ya wiki moja huduma hiyo imekuwa ikitolewa bure.

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospital ya Taifa ya Muhimbili Profesa Mohamed Janabi

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Profesa Mohamedi Janabi akiwahutubia wananchi wa kijiji hicho mara baada ya kufika kwenye kituo cha Afya Mtakanini na kupokelewa na umati mkubwa wa wanachi alisema kuwa nia ya serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wanapata hudua nzuri ya afya kuanzia kwenye zahanati,vituo vya afya ,hospitali za Wilaya na Hospitali za Rufaa ikiwemo hospitali ya Taifa Muhimbili .

Profesa Janabi ambaye ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema kuwa kila mtu anapaswa kutunza afya yake kwa kula vyakula ambavyo si hatarishi kwa afya jambo ambalo limekuwa likipigiwa kelele ili wananchi waweze kuacha kula vyakula bila kufuata utaratibu.

Alisema kuwa ni vyema kuacha kula vyakula vyenye sukari nyingi kwani sukari haija wahi kumuacha mtu salama hivyo ni vyema kuona umuhimu wa kuepuka kula vyakula vyenye sukali nyingi.

Baadhi ya wagonjwa waliokuja kuangalia afya zao katika kituo cha afya cha Mtakanini
Kituo cha afya cha Mtakanini kilichopo Halmashauri ya Namtumbo
Please follow and like us:
Pin Share