Vita vya kibiashara vilivyosababishwa na sera mpya za ushuru za rais Donald Trump wa Marekani vimeutawala mkutano wa mawaziri wa mambo ya nje wa nchi za BRICS unaofanyika mjini Rio de Janeiro, Brazil.
Mawaziri wa mambo ya nje wa Brazil, China, Urusi na nchi nyingine wanachama wa muungano wa BRICS wanaendelea na mazungumzo yao kwa siku ya pili leo mjini Rio de Janeiro yanayolenga kutafuta msimamo wa pamoja dhidi ya sera za kibiashara za Rais wa Marekani, Donald Trump.
Wanadiplomasia wakuu wa nchi 11 wanachama wa jumuiya ya kiuchumi ya BRICS wanakutana kwa mkutano wa siku mbili ulioanza jana kuandaa ajenda ya mkutano wa kilele wa wakuu wa nchi utakaofanyika mwezi Julai.
Waziri wa mambo ya nje ya Brazil Mauro Vieira amesisitiza umuhimu wa mdahalo katika wakati ambapo kunashuhudiwa migogoro ya kibinadamu, mizozo ya kivita, kuyumba kwa hali ya kisiasa na kumomonyoka kwa siasa za pande mbalimbali.
Waziri huyo pia amesema jukumu la BRICS ni muhimu zaidi wakati huu kuliko awali.
