Mashambulizi ya makombora na droni yamesababisha vifo vya watu watatu katika eneo linalokaliwa na Urusi katika mkoa wa Kherson. Shirika la habari la Urusi RIA limesema watu hao ni mwanamke na mtoto mmoja ambao waliuawa baada ya gari la wagonjwa kushambuliwa katika kijiji cha Mala Lepetykha huku mtu mwengine akiuawa katika kijiji cha Oleshky.
Kwa upande wake, Jeshi la Ukraine limesema limedungua droni zipatazo 107 kati ya 208 zilizorushwa na Urusi usiku wa kuamkia leo huku zingine 97 zikishindwa kufikia shabaha yao kutokana na ufanisi wa mifumo ya ulinzi wa anga.
Aidha, idara ya usalama ya Urusi FSB imefahamisha leo kuwa imezuia jaribio la Ukraine la kumuua kiongozi mkuu wa kanisa la Othodoksi la Urusi aliyefahamika kwa jina la Tikhon Shevkunov, 66, ambaye pia ni mjumbe wa baraza la ushauri la rais Vladimir Putin anayehusika na masuala ya utamaduni na sanaa.
(Vyanzo: Mashirika)
