Na Mwandishi wetu, JamhuriMedia, Tanga
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imewataka waandishi wasaidizi na waendesha vifaa vya Bayometriki
kutoa huduma bora kwa wananchi watakaojitokeza katika zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura linalotaraji kuanza Februari 13 hadi 19, 2025 katika mikoa ya Tanga na Pwani.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele wakati alipotembelea mafunzo ya siku mbili ya waandishi wasaidizi na waendesha vifaa vya Bayometriki katika Halmashauri za Jiji la Tanga, Mji wa Korogwe pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe vijijini.
“Ninawasihi muwahudumie wateja wenu kwa umahiri na unyenyekevu, msiwe na hasira kwani miongoni mwa wateja mtakao kuwa mnawashughulikia wengine ni wavijijini na wengine ni wamjini hivyo kila mtu anauelewa wake,” alisema Jaji Mwambegele.
Jaji wa Rufaa Mwambegele amesema ni jukumulao kuwaelishisha juu ya nini cha kufanya na wakawaeleze kwa upole na si kuwawakali bali kuwasaidia kuwaelekeza kwa unyenyekevu ili zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Wapiga Kura liweze kufanikiwa vyema kama ilivyo kusudiwa.
Aidha, akizungumza na washiriki hao akiwa Jijini Tanga, Jaji Mwambegele amewataka washiriki
hao kuwa waadilifu na kufanya kazi hiyo muhumu kwa taifa kwa moyo na kujituma.
Amewataka pia kutunza vifaa vyote watakavyo kabidhiwa wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo ili vifaa hivyo vilivyonunuliwa kwa gharama kubwa vikaweze kutumika katika maeneo mengine pindi vikitunzwa vyema.
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-42.png)
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika mkoani Tanga na Pwani kwa siku saba kuanzia tarehe 13 hadi 19 Februari, 2025 ambapo wapiga kura wapya 431,016 wanatarajiwa kuandikishwa na zoezi hilo litakapokamilika mikoa hiyo itakuwa na wapiga kura 2,727,318 sawa na ongezeko la asilimia 18.7 ya wapiga kura 2,296,302 waliopo kwenye daftari katika mikoa hiyo.
Mkoa wa Tanga zoezi la Uboreshaji litafanyika kwenye Halmashauri ya Jiji la Tanga, Halmashauri za Miji ya Handeni na Korogwe na Halmashauri za Wilaya ya Kilindi, Lushoto na Muheza na vituo vitafunguliwa saa 2:00 asubuhi na kufungwa Saa 12:00 jioni kila siku kwa siku saba.
Tume imeshakamilisha zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye mikoa 27 ya Kigoma, Tabora, Katavi, Geita, Kagera, Mwanza, Shinyanga, Mara, Simiyu, Manyara, Dodoma, Singida, Mjini Magharibi, Kusini Unguja, Kaskazini Unguja, Kusini Pemba, Kaskazini Pemba, Arusha, Kilimanjaro, Mbeya, Iringa, Rukwa, Songwe, Njombe, Ruvuma, Lindi na Mtwara.
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-38.png)
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-39.png)
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-40.png)
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-41.png)