Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es salaam

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw.Plasduce Mbossa amesema kuwa mamlaka hiyo imejipanga kufanya upanuzi wa bandari zake, ili kuweza kuendelea kutoa huduma shindani katika soko la Afrika na kimataifa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Huduma kwa Wateja Bw ambayo imeanza jana, Mbossa amesema kuwa mpaka sasa mamlaka hiyo imejiweka katika nafasi nzuri zaidi ya kiushindani kutokana na uwekezaji wake unaoendelea katika bandari mbalimbali hapa nchini, ikiwa ni pamoja na mpango wa kupanua na kujenga gati 10 katika bandari ya Dar es salaam ili kuongeza ufanisi na tija katika bandari hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mbossa akiwasikiliza wateja waliofika katika ofisi za TPA Jijini Dar es Salaam, jana ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Wateja.

“Katika kuhakikisha wateja wetu wanaendelea kupata huduma bora na stahiki sisi kama mamlaka tumekuja na mpango wa kuongeza gati 10 katika bandari ya Dar es salaam,”

“Hii inaenda kupanua soko la biashara kwa watumiaji wa bandari yetu kwani ufanisi utakuwa ni mkubwa na utakidhi mahitaji ya wateja wetu”, amesema.

Aliongeza kusema TPA imeendelea kuboresha miundombinu ya bandari zake ambazo ni pamoja na bandari ya Bagamoyo, Bandari ya Tanga, Mtwara, Mbamba Bay na bandari zingine ambazo ziko chini ya mamlaka hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mbossa akiteta jambo na Meneja Huduma kwa Wateja kutoka Kampuni ya Tanzania East Africa Getway Terminal Limited (TEAGTL), Bw. Abraham Kilyinga (kushoto) wakati wa hafla fupi ya maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Wateja iliyofanyika jana, makao makuu ya TPA Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Bw. Donald Tawala Mkuu wa Shughuli za Kampuni TEAGTL.

Amesema hayo yote yanafanyika ili kuhakikisha kuwa TPA inachochea uchumi wa Taifa kupitia Bandari zake kwa kushirikiana na wawekezaji waliopo.

“TPA tumejipanga kuufungua uchumi wa Taifa kwa kutumia bandari zetu na ndio maana tumeendelea kuboresha maeneo mengi ya bandari zetu ili ziweze kutoa huduma kwa wateja wetu wa ndani na nje ya nchi”

“Kwa kupitia uwekezaji ambao tumeufanya katika bandari zetu, matunda yake tumeanza kuyaona ambapo hadi sasa kumekuwa na utofauti mkubwa wa katika huduma za bandari ukilinganisha na miaka kadhaa ya nyuma”

“Hii inatokana na juhudi za Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuleta mageuzi makubwa ya kiutendaji katika bandari zetu ili kuchochea biashara zaidi na kukuza uchumi wa nchi yetun”amesema Bw. Mbossa

Amesema kuwa hadi kufikia sasa sekta ya uchukuzi inachangia zaidi ya asilimia 7.3 ya pato la Taifa ikiwa malengo yaliyopo ni kufikisha asilimia 15 .

“ili kufikia malengo, TPA tumeanza kuungana na makampuni makubwa ya meli duniani ili kuhakikisha bidhaa zinakuja kwa wingi na kwa bei rahisi ili kuwarahisishia na kutanua wigo wa kibiashara na mataifa ya jirani “

“Pamoja na maboresho ya bandari zetu, TPA imeendelea kuboresha mifumo ya malipo hasa katika mfumo wa kidijitali ambayo itamuwezesha mteja kulipia bidhaa au mzigo wake popote alipo badala ya kwenda ofisini.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mbossa akizungumza na Mkuu wa Shughuli za Kampuni kutoka Kampuni ya Tanzania East Africa Getway Terminal Limited (TEAGTL), Bw. Donald Tawala (kushoto) wakati wa hafla fupi ya maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Wateja iliyofanyika jana, makao makuu ya TPA Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Meneja Huduma kwa Wateja, Bw. Abraham Kilyinga.

Pia Bw. Mbossa aliwataka wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi kuendelea kutumia bandari za Tanzania katika kusafirisha mizigo yao kwani ufanisi uliopo kw asasa katika bandari hizo ni mkubwa ukilinganisha na awali.

Naye Mkuu wa shughuli za kampuni ya kampuni ya Tanzania East Africa Getway Terminal Limited (TEAGTL) Donald Tawala amesema kuwa Bandari imekuwa ikifanya maboresho katika maeneo tofauti tofauti, hivyo wao kwa kushirikiana na TPA wameendelea kufanya mageuzi makubwa katika uboreshaji wa huduma wanazozitoa ikiwa ni pamoja na uboreshaji wa mifumo ya malipo, uboreshaji wa mifumo ya kupakia na kushusha mizigo katika meli , na lengo mageuzi hayo ni kuhakikisha ufanisi katika bandari unaongezeka na kuwa na tija.
Mwisho

Please follow and like us:
Pin Share