Mbioni kupata Ithibati

Maabara ya Tume ya Madini sasa imetambulika rasmi kisheria na ipo mbioni kukamilisha mchakato wa kupata Ithibati.

Maabara hiyo ya Tume ya Madini iliyopo Msasani jijiini Dar es Salaam ambayo kwa sasa inatambulika kisheria inafanya kazi ya uchunguzi wa sampuli za madini, udongo na miamba.

Akizungumza leo Machi 3, 2025 kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini katika kikao kazi mkoani Morogoro, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira wa Tume ya Madini, Mhandisi Hamisi Kamando, amesema kwa sasa Maabara ya Tume ya Madini ina nguvu kisheria hivyo itaongeza nguvu ya ukusanyaji wa maduhuli ya serikali na kuwarahisishia wadau wa sekta ya madini kupima sampuli zao kwa haraka.

“Lengo la maabara ya Tume ya Madini ni kuhakikisha serikali inapata stahiki zake. Pia inafanya biashara ya kupima sampuli za wateja na kuongeza pato la serikali,”amesema.

Awali, akizungumza, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini, Venance Kasiki amesema Maabara ya Tume ya Madini kwa sasa inatambulika kisheria kupitia ‘Written Laws (Miscellaneous Amendments Act, 2024)

’“Kutambulika kwa maabara yetu kisheria inatupa faraja ya kuongeza ari ya kufanya kazi,”amesema Kasiki na kuongeza,

“Idara ipo kwenye hatua mbali mbali za kukamilisha mchakato wa kupata ithibati,”amesema.

Amesema, mojawapo ya hatua hizo ni Management Review, hivyo wameandaa kikao cha ‘Management Review’ ikiwa ni moja kati ya takwa la kuwezesha Maabara Kupata Ithibati ISO/IEC 17025:2017.

“Katika kikao hiki tumeeleza hatua mbalimbali zitakazo wezesha Maabara kupata Ithibati, na mahali tulipo kwa sasa na tunapokwenda katika safari ya kupata ithibati,” amesema Kasiki.