Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Shahidi Kiran Lalit Ratilal (52), ameileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam jinsi mume wake alivyopigwa na mshtakiwa Bharat Nathwan (57) hadi kupoteza fahamu kutokana na ugomvi ambao ulikuwa unaendelea wa baina yao kuhusu ujenzi uliyokuwa unaendelea katika eneo la makazi yao.

Nathwan pamoja na mke wake Sangita Bharat (54) wanaoishi Mtaa wa Mrima – Kisutu, jengo la Lohana Dar es Salaam wanatuhumiwa kwa mashtaka manne likiwemo la kujeruhi waliyoyatenda Julai 21,2023 kinyume cha sheria.

Akiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Grace Mwanga, Kiran alidai kuwa anakumbuka Julai 21, 2023 alikuwa nje ya akiendelea na majukumu yake nanpia shughuli za mapambo zilikuwa zinaendelea nyumbani kwake mafundi wakiweka vigae.

Alidai kuwa, mshtakiwa Sangita alitoka ndani akaanza kupaza sauti akitaka atoe malighafi (material) yote yaliyokuwepo kwenye kibaraza hicho, wakati yote yapo upande wa Kiran Lalit Ratilal na sio upande wake.

“Aliendelea kupaza sauti mimi nikamjibu kwamba nitaondoa baada ya mafundi kumaliza kazi, nilipomjibu akaanza kutumia lugha chafu akidai hataki kusikia chochote na kwamba niondoe uchafu wangu,”

“Nilijaribu kumuelewesha, lakini hakunielewa ndipo nilipompigia simu mume wangu akakuchukua dakika tano aafika pale, wakati anafika na mume wa mshtakiwa Sangita nae akafika kwa maana ya Bharat,”alidai Kiran.

Kiran alidai kuwa baada ya waume zao kufika kwa pamoja, akajaribu kumuelewesha Bharat kutokana na aliyoyasema mke wake (Sangita), lakini hakumulewa na pia mume wake alijaribu kuwaelewesha nankuwataka wakayazunguze lakini hawakuelewa.

“Sangita alianza kutumia maneno machafu tena, na nilipomuelewesha mume wake kuhusu maneno machafu ya mke wake alikaa kimya, mume wangu akaniambia kama hawajamuelewa awaache,”alidai

Alidai kuwa baada ya kumalizia hiyo sentensi, Bharat alimrukia mume wake na kuanza kumpiga kwa kumkandamiza kifuani na kumpiga mateke.

“Aliendelea kumpiga mume wangu nilipoenda kuamulia Bharat alinishika kichwa changu na kukitumbukiza kwenye ndoo ambayo ilikuwa na mchanganyiko wa saruji na kisha akaendelea kumpiga mateke,”

” Watu wote waliyokuwepo kwenye eneo hilo wakaanza kumsukuma Bharat ndipo alipoanicha mimi na kumfuata tena mume wangu akaanza kumpiga akadondoka chini akapoteza fahamu, muda huo uso wangu, macho na masikio yalikuwa yamejaa saruji ila nilikimbia kumsaidia ila hakuweza kuamka,”alidai Kiran

Kiran alidai kuwa alimuita mtu wa ofisini ili aweze kumsaidia ndipo alipompa simu yake akaanza kuchukua picha, mshtakiwa Sangita baada ya kuona hivyo alichukua simu hiyo ili aitupe wakati hayo yote yanaendelea mume wake alikuwa amelala chini.

“Nilifikiria njia ya kumsaidia mume wangu, mafundi walimbeba hadi sakafu ya pili ndipo akaanza kuzinduka akapewa maji, wakamkimbiza hospitali kwa ajili ya kupata huduma ya kwanza. Niliondoa saruji baada ya mume wangu kuzinduka, aliulizia simu yake akaanza kupiga simu,”

“Niliona wanaume wawili wakiwa wamevaa nguo za polisi, taratibu macho yangu yakaanza kupoteza uono kwa sababu ya ule mchanganyiko. Waliniambia natakiwa niende Kituo cha Polisi Kati kuripoti wakanishauri niite gari la wagonjwa kwa sababu nilikuwa siwezi kutembea vizuri,”alidai

Alidai alifanikiwa kuita gari hilo, wakati hayo yote yakiendelea Bharat aliendelea kutoa maneno machafu na za kitishio ya maisha, gari hilo lilimpeleka hadi kituoni hapo akapewa fomu moja akiwa na mume wake akampelekwa Hospitali ya Mnanzi Mmoja kwa matibabu.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 6,2024, baada ya Wakili wa washtakiwa hao Edward Chuwa kuomba ahirisho kwa sababu alikuwa anakwenda kwenye shauri lingine mahakama ya juu, siku atamuuliza maswali ya dodoso shahidi.

Please follow and like us:
Pin Share