Naibu Waziri Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Dk. Festo Dugange, ameagiza ofisi za halmashauri kuhakikisha vifaa vya kujifungulia vinapatikana katika vituo vya afya.

Akijibu swali bungeni mjini Dodoma, Dk. Dugange alisema kwamba sera ya afya inatoa muongozo wa huduma kwa wakinamama wajawazito, ambapo wanatakiwa kupatiwa huduma bure. “Naelekeza kwa halmashauri zote nchini ni maelekezo ya serikali na kauli ya serikali kuhakikisha vifaa vyote vya kujifungua vinapatikana katika vituo vyote,” alisema Dk. Dugange.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Dk. Dugange alifafanua kuwa katika bajeti ya mwaka huu wa fedha 2025/2026, serikali imepanga kutumia shilingi milioni 265 kujenga jengo la upasuaji na wodi ya wakinamama katika Wilaya ya Nsimbo.

Dk. Dugange aliongeza kuwa serikali itaendelea kutoa ajira kwa watumishi wa afya ili kuziba pengo la upungufu wa watoa huduma wa afya katika maeneo mbalimbali nchini.