*Asisitiza kuwa mifugo ni uchumi, ajira na biashara

*Atoa wito kwa wakulima na wafugaji wawe wamoja

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha sekta ya mifugo inakuwa endelevu na yenye tija.

Amesema kuwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan mara zote ameweka msisitizo katika kuiendeleza sekta hiyo kwa kuwa mifugo ni uchumi, ajira na ni biashara.

Ameyasema hayo kwa nyakati tofauti alipozungumza na wananchi katika mikutano aliyoifanya jana Jumatano (Machi 12, 2025) Wilayani Igunga, mkoani Tabora ambapo yupo kwenye ziara ya kikazi ya siku mbili.

“Tunawahamasisha wafugaji, fugeni mifugo ni uchumi, mifugo ni maisha na mifugo ni pesa na wakulima limeni tupate mazao mengi ya chakula na biashara na ni lazima wafugaji na wakulima tuelewane.”

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari Seif Gulamali katika  jimbo la Manonga wilayani Nzega, Machi 12, 2025. Wa pili kushoto ni Mbunge wa Manonga, Seif Gulamali na kulia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Nassoro Hamdan.  (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Katika hatua nyingine Mheshimiwa Majaliwa amezitaka halmashauri zote nchini kuweka mikakati ya kuhakikisha wanakuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na kuzisimamia fursa zilipo kwenye maeneo yao ili kuwanufaisha wananchi. “Mkifanya hivyo mtakuwa mmewasaidia wananchi kujiendeleza kiuchumi.”

Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi kwenye shule ya Sekondari ya Seif Gulamali, Mheshimiwa Majaliwa ameitaka jamii kuweka nguvu za pamoja katika kumlinda mtoto wa kike ili waweze kutimiza ndoto zao.

Pia, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa mikakati iliyopo katika sekta ya elimu ili sekta hiyo iweze kuwanufaisha watanzania kwa kukuza ubora wa elimu nchini.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipokelewa na viongozi alipowasili kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Seif Gulamali katika  jimbo la Manonga wilayani Nzega kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule hiyo, Machi 12, 2025.  (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akiwasalimia wananchi baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari Seif Gulamali iliyopo katika jimbo la Manonga wilayani Igunga, Machi 12, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia wananchi alipowasili kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Seif Gulamali katika  jimbo la Manonga wilayani Nzega kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule hiyo, Machi 12, 2025.  (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)