Rubani mmoja amefariki baada ya helikopta kuanguka kwenye paa la hoteli moja katika mji wa Cairns kaskazini mwa Queensland.

Ndege hiyo ilianguka kwenye hoteli ya DoubleTree mwendo wa 01:50 usiku kwa saa za eneo hilo siku ya Jumatatu, na kuwaka moto ambapo mamia ya wageni walihamishwa eneo salama.

Mamlaka inasema mtu pekee aliyekuwa kwenye helikopta hiyo ndiye aliyefariki katika eneo la tukio, huku wageni wawili wa hoteli hiyo – mwanamume mwenye umri wa miaka 80 na mwanamke mwenye umri wa miaka 70 – walipelekwa hospitalini na wako katika hali nzuri.

Polisi wa Queensland na waangalizi wa usalama wa anga wanachunguza mazingira ya ajali hiyo, huku kampuni inayokodisha helikopta hiyo ikisema ilikuwa katika safari ambayo “haikuidhinishwa”.

Amanda Kay, ambaye alikuwa akiishi katika hoteli kwenye eneo kuu la esplanade huko Cairns, alielezea kuona helikopta ikiwa eneo la “chini zaidi”, bila taa katika hali ya hewa ya mvua.

“[Imegeuka] na kuanguka kwenye jengo,” alisema, akiongeza kuwa ndege “iliwaka moto”.

Mtu mwingine alisema aliona helikopta hiyo ikipita karibu na hoteli hiyo mara mbili kabla ya kuanguka.

Please follow and like us:
Pin Share