-Aitaka jamii kuacha kushabikia vitendo vinavyodharirisha utu wa binadamu

-Asema mtoto anasitahili kulindwa na kupatiwa haki yake

-Atoa rai kwa jamii kuacha tabia za kibaguzi kwa watoto wenye ulemavu

na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila leo Juni 20,2024 ameshiriki maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika akiwa mgeni rasmi katika viwanja vya Karimjee Jijini Dar es Salaam

Akiwa katika viwanja vya Karimjee RC Chalamila alipata wasaa wa kutembelea maonyesho ya kibunifu katika mabanda mbalimbali yaliyoandaliwa katika viwanja hivyo.

Mhe Mkuu wa Mkoa akiongea wakati wa maadhimisho hayo ameitaka jamii kuacha kushabikia vitendo vinavyodharirisha utu wa binadamu kwa mfano tabia ya biashara ya ngono inafanywa na baadhi ya wanawake maarufu kwa jina la “Madada Poa” biashara hiyo imekuwa ikifanyika hadharani bila kujali mila na tamaduni za kiafrika, malezi ya watoto yamekuwa hatarini kutokana na tabia hizo hivyo siyo vema hata kidogo jamii kushabikia vitendo hivyo “ Katika Mkoa wa Dar es Salaam tabia za biashara za ngono hazikubariki “ amesema RC Chalamila.

Aidha RC Chalamila amesema wakati tunaadhimisha siku ya mtoto Afrika ni vema kutafakari na kujikumbusha wajibu wetu kama jamii katika mambo mbalimbali ikiwemo makuzi na malezi ya mtoto bila kusahau mtoto anastahili kulindwa na kupatiwa haki yake stahiki

Vilevile RC Chalamila ameitaka jamii kuacha tabia ya kubagua watoto wenye ulemavu ambapo amesema Rais Dkt Samia ni kielelezo kizuri kwa kuwa amekuwa mstari wa mbele kuwekeza katika elimu Jumuishi na hata katika teuzi zake watu wenye ulemavu wamekuwa wakiteuliwa pia kwenye Ajira wamekuwa wakipewa fursa sawa na watu wasio na ulemavu.

Sanjari na hilo RC Chalamila ameelekeza maadhimisho yajayo yafanyike kwa ukubwa zaidi ili kutoa fursa kubwa kwa watoto kufurahia siku hiyo ikiwemo kuwepo kwa michezo ya watoto ya aina mbalimbali

Ifahamike kuwa maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika hufanyika kila mwaka Juni 16 ambapo huambatana na shughuli mbalimbali za watoto ikiwemo miadahalo kwa lengo la kutathimini changamoto na mafanikio katika mchakato mzima wa makuzi na malezi ya mtoto unaozingatia kulindwa na kupatiwa haki yake

Please follow and like us:
Pin Share