Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila leo Julai mosi,2024 amekutana na Kamati ya Ardhi Mali asili na Utalii katika ukumbi wa mikutano wa ofisi hiyo Ilala Boma

Kamati hiyo ya Bunge ikiongozwa na mwenyekiti wake Timotheo Paul Mnzava iko katika ziara ya kikazi katika Mkoa wa Dar es Salaam ambapo jana Juni 30,2024 ilitembelea miradi NHC kawe na Moroco Square na leo Julai mosi 2024 inaendelea na ziara Gongo la Mboto Ilala kukagua maendeleo ya mradi wa ukwamuaji wa zoezi la urasimishaji wa Ardhi.

Akiongea na kamati hiyo RC Chalamila ameipongeza kamati hiyo kwa namna inavyotekeleza majukumu yake na kufanya ziara katika Mkoa huo ambapo amesema mkoa huo bado unachangamoto ya migogoro ya Ardhi na ofisi yake inaendelea kutatua migorogoro hiyo.

Pia alizungumzia suala la maji kujaa nyakati za mvua ambapo amesema yeye hawezi kuita ni mafuriko kwa sababu sehemu nyingi zinazojaa maji ni zile ambazo zimejengwa kiholela na kuzibwa kwa mifereji ya maji hivyo ni vema upimaji na upangaji wa miji uakisi changamoto hiyo,vilevile amesema bado sekta ya utalii haijafanya vizuri lakini kwa upande wa Mkoa huu tayari Katibu Tawala wa Mkoa Dkt Toba Nguvila ameshaanza kulifanyia kazi kwa kushirikiana na mali asili.

Aidha kwa upande wa mwenyekiti wa kamati Mhe Mnzava amesema ni wakati muafaka wa kuwekeza katika urasimishaji kwa kuwa tayari makosa yalishafanyika hivyo urasimishaji ni kujisahisha, pia kwa Mkoa wa Dar es Salaam katika utalii ni lazima kuweka mikakati ya maksudi kwenye utalii wa fukwe na Hotel kwa kuwa wageni wengi hutembelea mkoa huu wa kibiashara.

Mwisho katika msafara huo wa kamati ya Bunge kwa upande wa wizara ya Ardhi walikuwepo wataalam wa wizara pamoja na Naibu waziri wa Ardhi, Mhe Pinda lakini pia wataalam wengine wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa akiwemo Katibu Tawala wa Mkoa Dkt Toba Nguvila.