📌Asema hekta 469,000 za misitu zinateketea kwa shughuli za binadamu

📌Asisitiza Nishati Safi ya Kupikia si anasa

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Maryprisca Mahundi amesema nchi inakwenda kushuhudia mageuzi makubwa ya utunzaji wa mazingira kupitia Mkakati wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambao kinara wake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mahundi ameyasema hayo jijini Dodoma wakati akihamasisha wananchi kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi na kuanza kupika kisasa kupitia nishati safi ya kupikia.

“Tunaposema tutunze mazingira, tunaweza kuona takriban hekta 469,000 za misitu zinateketea kwa mwaka sababu ya shughuli mbalimbali za binadamu ikiwemo matumizi ya nishati zisizo safi za kupikia (kuni na mkaa) hivyo tunapotumia nishati safi kupikia tunaenda kutunza mazingira yetu.” Ameeleza Mahundi.

Amesema mbali ya uharibifu wa mazingira ambao umekuwa ukitokea kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi lakini pia kumekuwa na athari kwa watumiaji hasa kuathirika mfumo wa upumuaji kutokana na moshi mwingi.

Ameongeza kuwa, zaidi ya watanzania 33,000 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi.

Ameeleza kuwa, katika matumizi ya nishati safi ya kupikia kama vile gesi na umeme kila aina ya chakula kinaweza kupikwa na kutilia mkazo kuwa nishati safi ya kupikia si anasa bali inaenda kulinda afya za watumiaji pamoja na mazingira.

Please follow and like us:
Pin Share