Na Lookman Miraji, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Pazia la maonyesho rasmi ya nishati kwa mwaka 2024 yamezinduliwa rasmi leo jijini Dar es Salaa ambapo yanakuwa ni maonyesho ya nane tangu yalipofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 2017.

Hafla ya ufunguzi wa maonyesho hayo imefanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee ulioko upanga, Dar es Salaam.

Shughuli hiyo ya ufunguzi iliongozwa na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Exaud Kigahe ambae aliwaongoza wawekezaji na wafanyabiashara wengine kutangaza biashara zao.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi wa maonyesho hayo Naibu Waziri Kigahe amesema kuwa lengo la maonyesho hayo ni kuona namna gani wanaweza kuendeleza nishati safi na ya kutosha lakini pia ya bei nafuu kwa Watanzania.

“Leo nimezindua rasmi maonyesho ya nane ya nishati ambapo lengo lake ni kuona namna gani tunaweza kuendeleza nishati safi na ya kutosha pamoja na kuwa ya bei nafuu kwa watanzania.

Kikubwa zaidi tunataka tuhamasishe zaidi uzalishaji wa nishati safi na jadidifu ambayo ni rafiki kwa mazingira ambayo miongoni mwake ni umeme wa jua (solar), umeme wa upepo pamoja na ule unaoweza kuzalishwa kutokana na mabaki ya kazi mbalimbali lakini zaidi kuna umeme unaotokana na Majina lengo hasa ni kupunguza uchafuzi wa mazingira katika kuzalisha umeme au nishati.” Alisema hayo naibu waziri Kigahe.

Mbali na hayo naibu Waziri Kigahe amegusia pia juu mambo ambayo Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza ni kuona namna gani ya kuwasaidia Watanzania kuwa na nishati ya kutosha ya kutumia katika majumba na viwanda pamoja na kuhakikisha wale wote ambao hawapati umeme kuwepo na nishati mbadala ambayo ni safi na ikiwemo gesi inayotumika kwa kupikia.

“Kupitia maonyesho haya wanawaasa Watanzania waje waone jinsi ambavyo kuna vyanzo vingi vya kuzalisha umeme na teknolojia rahisi ambazo zitatusaidia kuzalisha umeme jadidifu ambao tunaweza kutumia kwenye matumizi yetu ya nyumbani pamoja na viwandani.

Kwa hiyo naomba niwahamasishe Watanzania sasa tuanze kujifunza kutumia umeme ambao ni safi na salama na wa bei nafuu ambao unaweza ukazalishwa kupitia vyanzo mbalimbali vya jua, upepo pamoja na maji.” amesema Naibu Waziri Kigahe.

Aidha pia naibu Kigahe ameongeza kuwa Serikali kupitia maonyesho hayo kama sehemu ya kuifungua sekta ya uwekezaji kwa raia ya kigeni ambapo Serikali imelenga kutengeneza nishati ya kutosha ili kuwashawishi wawekezaji wa kigeni kuja kuwekeza nchini kwani miongoni mwa malengo mama ya Serikali ya Awamu ya Sita na ndio maana jitihada zinaendelea kufanyika kuhakikisha bwawa la mwalimu Nyerere linakamilika kwa haraka.

Kwa upande mwingine pia Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) kimeshiriki katika maonyesho hayo ambapo nao kupitia mtendaji wake Josephat Haule wameeleza kwa namna ambavyo wao wanaungana na Serikali kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya nishati.

Akizungumza na gazeti la Jamhuri Digital leo hii mtendaji huyo ameeleza kuwa wao pia wanawakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza nchini kwani kuna baadhi ya faida watakazozipata endapo wakisajili miradi yao katika kituo hicho.

Miongoni mwa faida ambazo amezielezea mtendaji huyo ni pamoja na unafuu wa gharama za kodi kwa mwekezaji endapo akiwa amesajiliwa na anatambulika na kituo hicho.

Katika maonyesho hayo kwa mwaka huu yamekutanisha kampuni mbalimbali zinazojishughulisha na utengenezwaji na usambazwaji wa nishati kutoka ndani na nnje ya nchi pia.

Maonyesho hayo yanatarajia kuendelea kwa siku mbili ambapo yatafungwa rasmi septemba 27 mwaka huu.

Please follow and like us:
Pin Share