Na. Abel Paul wa Jeshi la Polisi

Jeshi la Polisi nchini limesema kuwa limeendelea kupokea maswali toka kwa wanahabari na wananchi wa kada mbalimbali kufuatia matamshi ya Mhe.Abdulrahman Kinana, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara aliyoyatoa Julai 27,2023 huko Bariadi Mkoa wa Simiyu. Ambapo matamshi hayo Mhe.Abdulrahman Kinana yalinikuliwa yakisema watazungumza na kuishauri Serikali katika kupitisha sheria Bodaboda wabebe watu zaidi ya mmoja.

Akitoa taarifa hiyo leo Msemaji wa Jeshi la Polisi Nchini Kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi SACP David Misime amesema kuwa Wote wanaopiga simu wanataka kujua nini msimamo wa Jeshi la Polisi.

Misime amebainisha kuwa Kimsingi Jeshi la Polisi ni wasimamizi wa sheria zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo miongoni mwa sheria hizo ikiwa ni kifungu namba 59 cha Sheria ya Usalama Barabarani Sura 168 ambacho kinakataza pikipiki kubeba abiria zaidi ya mmoja.

Pia amebainisha kuwa hata hivyo Mhe Abdulrahman Kinana hakusema bodaboda wapakie abiria zaidi ya mmoja bali ‘wataenda kushauri’.

Mwisho Msemaji wa Jeshi hilo alisema kuwa tunawaelekeza bodaboda wafuate sheria iliyopo kwa sasa ambayo wanaisimamia yenye katazo hilo na endapo ushauri utakaotolewa utakubalika na sheria kubadilishwa basi tutasimamia sheria ya wakati huo, kwa sasa sheria ya kutopakia abiria zaidi ya mmoja iendelee kufuatwa na kuzingatiwa ipasavyo.

Hii itatusaidia sote kuendelea kuwa salama tunapotumia Barabara na vyombo hivyo Alisema Misime.

Please follow and like us:
Pin Share