Na Mwandisi Wetu,JamhuriMedia, Dar es Salaam

Waziri wa Afya Jenista Mhagama amesema miongoni mwa majukumu ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii ni kupima magonjwa yasiyoambukiza na yanayoambukizwa.

Amesema wahudumu hao watapita nyumba kwa nyumba katika vijiji mbalimbali vya mikoa 11 na vipimo kama vile vipimo vya Kisukari, Shinikizo la juu la damu, Udumavu, Malaria na vingine.

Akizungumza leo na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam amesema vipimo hivyo vya awali vitasaidia wananchi kupata upimaji wa awali na kujua afya zao na endapo watahitaji matibabu zaidi wataenda vituo vya afya.

“Kama kisukari akijua afya yake itasaidia na ambao walikuwa na tatizo wataanza matibabu mapema baada ya kwenda kwenye vituo vya afya,niwaombe wananchi kwasababu watawatembelea na kupima na kutoa ushauri wa kiafya waachwe wafanya kazi zao iliyokusudiwa,” amesisitiza.

Ameongeza “Tutawapa vifaa vya kupima malaria haraka wanaweza kutoa dawa za awali za ugonjwa wa malaria pia lakini hapo hapo wataelekezwa kwenda kwenye vituo vya afya.

Amebainisha kuwa majibu yatakuwa siri ya mtu lakini mwanajamii atashauriwa kwenda vituo vya afya na pia wahudumu watapewa Vishkwambi kwaajili ya kukusanya taarifa.

“Na kuna kipimo cha udumavu watoto watapimwa kwenye mkono kama wanaudumavu itaonesha ni kipimo rahisi,tutawapa mavazi maalum na viatu ,koti la mvua na tumeweka utaratibu wa vifaa vingine muhimu.

Amesema Serikali imetenga Sh bilioni moja kwa ajili ya mpango huo huku mikoa 11 ambayo zoezi hilo litafanyika ni Geita,Mbeya,Tanga,Songwe,Lindi,Tabora, Kagera, Njombe, Ruvuma, Pwani na Kigoma.

Aidha jumla ya wahudumu 11,514 watatoa huduma ambapo kwa kila mtaa au kitongoji watukuwepo wahuduma wawili wanaotoka katika jamii hizo.

Please follow and like us:
Pin Share