Na Dotto Kwilasa,JamhuriMedia,Dodoma

Katika kufanikisha huduma kwa wanachama wa Mfuko wa Taifa wa bima ya afya (NHIF) na Mfuko wa huduma za afya Zanzibar (ZHSF) zimesaini mkataba wa makubaliano wa mashirikiano katika utoaji wa huduma kwa wanachama wake ili kuongeza wigo mpana wa vituo vya kutolea huduma vilivyosajiliwa na NHIF nchi nzima.

Hatua hii inatajwa kuwa itasaidia wananchi na wakaazi wote wa Zanzibar kutokuwa na kikwazo cha fedha pale wanapozihitaji huduma ya afya pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa rasilimali fedha za kutosha katika kugharamia huduma hiyo.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa NHIF Bernard Kongaku kupitia uzoefu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), katika uendeshaji wa mfumo wa bima ya afya nchini, Julai Mosi, 2024 ZHSF itaanza rasmi majukumu yake kwa kuhudumia wanachama na wategemezi wake kupitia Vituo vya kutolea huduma vilivyosajiliwa na NHIF Tanzania Bara.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo June 28,2024 Jijini Dodoma,Konga amesema katika maandalizi yaliyofanywa na NHIF utayari wa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa mashirikiano umefanyika ili kuhakikisha wanachama hao wanapata huduma bila ya changamoto yoyote.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa ZHSF Yaasin Juma amesema hatua hiyo itahakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi na wakaazi wote wa Zanzibar na kuhakikisha upatikanaji wa rasilimali fedha za uhakiki na endelevu kwa kugharamia huduma za afya.

“Taasisi hii ilianza utekelezaji wa majukumu yake kwa kuanza na usajili wa wanachama wa Sekta ya umma mwezi wa Julai,2023 na Oktoba, 2023 huduma za matibabu kwa vituo vilivyosajiliwa na ZHSF zilianza kutolewa rasmi kwa upande wa Zanzibar, ” Amesema

Amefafanua kuwa Mwezi wa Machi, 2024 ZHSF ilianza usajili wa sekta Binafsi na huku tukiandaa mikakati ya kuelekea katika usajili wa sekta isiyo rasmi na makundi mengine yasiyokuwa na uwezo kama ilivyoelekezwa katika Kifungu cha 2 cha Sheria ya Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar Nam.1 ya 2023.

Katika kipindi cha mpito cha kuwafikia wanachama walioko Tanzania Bara,amefafanua kuwa watashirikiana na NHIF ili kuweka utaratibu wa muda wa kuwawezesha wanachama hao kupata huduma za afya, ambapo ZHSF ilikua ikilipa michango ya wanachama hao NHIF.

“Vilevile, ZHSF na NHIF zilikua zikishirikiana kwa wanachama wote ambao kabla ya kuanzishwa kwa ZHSF walikua ni wanachama wa NHIF ambapo hadi sasa NHIF inaendelea kuwapatia huduma wanachama hao kwa kutumia kadi za NHIF, ” amefafanua na kuongeza;

Kwa mujibu wa kifungu cha 27 cha Sheria Nam.1 ya 2023, Mfuko umepewa uwezo wa kuwafikishia wanachama wake huduma za afya nje ya Zanzibar, ambapo kwa kuanzia ZHSF imeanza kuwafikia wanachama wake walioko Tanzania Bara. Tukio la leo linaakisi utekelezaji wa masharti ya Sheria hiyo, “anasiaitiza Mkurugenzi huyo.

Pamoja na Mambo mengine amesema, “mafanikio haya ya kufikia makubaliano na wenzetu wa NHIF ni ya kujivunia kwani yatawawezesha wanachama wetu kupata huduma za afya wakiwa Tanzania Bara kwa kutumia kadi za ZHSF, ” amesema.

Amesema wanategemea mashirika ya ZIC, PBZ ambayo yanafanya kazi Tanzania Bara na wategemezi ambao wachangiaji wao wapo Zanzibar watafaidika na huduma hizo.

“Kuanzia mwezi wa Julai, 2024 watumishi ambao walikuwepo NHIF kutoka sekta ya umma watarudi rasmi ZHSF na wafanyakazi wote waliopo sekta binafsi wataanza kupata huduma ZHSF kuanzia tarehe 1 Septemba, 2024. Vilevile ZHSF itafungua ofisi Tanzania Bara ili kuratibu kwa ukaribu maswala yetu”amesema.