Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio amesema mchakato wa serikali ya Rais Donald Trump wa kusitisha misaada kupitia Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la USAID umekamilika.

Kwenye mtandao wa X, Rubio amesema baada ya wiki sita za mapitio, sasa wanafuta asilimia 83 ya programu zilizofanywa chini ya shirika hilo la USAID.

Amesema mikataba 5,200 ambayo sasa imefutwa, ilitumia mabilioni ya dola kwa namna ambazo hazikuwa na manufaa yoyote kwa taifa la Marekani.

Ameongeza kuwa karibu mikataba 1,000 iliyobakia itaratibiwa moja kwa moja na Wizara yake.