Marekani inachunguza uvujaji wa nyaraka za siri zinazoelezea tathmini ya Marekani kuhusu mipango ya Israel kushambulia Iran

Spika wa Baraza la Wawakilishi Mike Johnson amethibitisha.

Nyaraka hizo ziliripotiwa kuchapishwa mtandaoni wiki iliyopita na zinasemekana kuelezea picha za satelaiti zinazoonyesha Israel ikihamisha zana za kijeshi kwa ajili ya kujiandaa kukabiliana na shambulio la kombora la Iran tarehe 1 Oktoba.

Nyaraka hizo, ambazo ni siri kuu, zinaweza kusambazwa ndani ya muungano wa mashirika ya kijasusi wa ‘Five Eyes’ wa Marekani, Uingereza, Kanada, New Zealand na Australia, CBS.

Kwa wiki kadhaa Israel imekuwa ikiamua jinsi na wakati wa kujibu shambulio la hivi punde la kombora la Iran. Waziri wa ulinzi wa Israel ameonya kuwa litakuwa “Kali, sahihi na la kushangaza”.

Nyaraka hizo mbili zinaripotiwa kuhusishwa na Shirika la Kitaifa la Ujasusi la Geospatial la Marekani na Shirika la Usalama wa Taifa (NSA), na zilichapishwa kwenye akaunti ya Telegram inayofungamana na Iran siku ya Ijumaa.

Johnson, mwanachama wa ngazi ya juu zaidi wa Congress, aliiambia CNN Jumapili kwamba “uvujaji huo unatia wasi wasi sana”.

“Kuna madai mazito yanayotolewa, uchunguzi unaendelea, na nitapata maelezo mafupi juu ya hilo baada ya saa chache,” mjumbe huyo wa Republican wa Louisiana alisema.

Pentagon ilithibitisha katika taarifa yake kwamba inafahamu ripoti kuhusu hati hizo, lakini haikutoa maoni zaidi.

Mashirika ya Marekani yanayohusika, pamoja na serikali ya Israel, hazijatoa maoni yao hadharani kuhusu uvujaji huo.

CNN na Axios kwanza ziliripoti uvujaji huo, ambao unathibitisha kwa mara nyingine tena kwamba Marekani huichunguza mshirika wake wa karibu Israel.

Hati moja inarejelea uwezo wa nyuklia wa Israeli – ambayo Marekani na Israel kamwe hawajakiri rasmi – na kufutilia mbali matumizi ya chaguo kama hilo katika shambulio lolote lililopangwa .

Afisa mmoja wa zamani wa ujasusi wa Marekani aliiambia BBC kuwa kutolewa bila kibali kwa hati hizo pengine ni jaribio la kufichua ukubwa wa ulipizaji kisasi uliopangwa, kwa lengo la kuuvuruga.

Marekani inachunguza iwapo taarifa hizo zilifichuliwa kimakusudi na ajenti wa Marekani, au iwapo ziliibwa, pengine kwa njia ya udukuzi, maafisa waliambia Associated Press (AP).

Nyaraka hizo mbili zinaonekana kutegemea taarifa za satelaiti zilizopatikana kuanzia tarehe 15-16 Oktoba.