
📌 Wamshukuru Rais Samia kwa kupunguza gharama za umeme
📌 Elimu kuhusu matumizi bora ya nishati yatolewa
📌 Watakiwa kuchangamkia fursa ya kuunganisha umeme
Wananchi mkoani Mara wamesisitiza kuridhishwa na utekelezaji miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), inayotekelezwa nchini kwa lengo la kuwapatia umeme wa gharama nafuu, na wameipongeza Serikali kwa kuwafikishia miradi hiyo muhimu yenye faida kwa uchumi wa Taifa.
Pongezi hizo zimetolewa na wananchi kwa Wataalam wa REA waliofika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kutumia fursa ya miradi ya REA inayotekelezwa katika Kata ya Kwangwa wilaya ya Musoma mkoani Mara.

Aidha, wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuipatia fedha REA kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya umeme mkoani humo.
Awali Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka REA, Abdulrazack Mkomij ametoa elimu kwa umma kuhusu gharama za kuunganisha umeme, matumizi bora ya nishati, kuhamasisha kuunganisha umeme, tahadhari za umeme na elimu kuhusu utunzaji wa miundombinu ya umeme.
Naye, Mhandisi wa Miradi ya REA mkoa wa Mara, Omary Gwillah, amesema kuwa REA inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme mkoani humo ili wananchi wafanye shughuli zao kwa tija.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Kata ya Kwangwa, Bwiso Kinanda, ameishukuru Serikali kwa kupunguza gharama za uvutaji umeme. Amewataka wananchi kutumia fursa hiyo ya uvutaji wa umeme.
Vile vile, Mwenyekiti wa Mtaa wa Kwangwa B, Maxmilian Kunju akizungumza kwa niaba ya wananchi ameiomba REA kuendelea kufikisha umeme kwenye maeneo mengine mkoani humo ili wananchi wa Musoma wapate nishati ya umeme.


