Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Pwani

Serikali mkoani Pwani ,imehimiza wananchi kutoa maoni yao ili kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025-2050 kwa manufaa ya vizazi vijavyo pamoja na kuwa na Tanzania yenye Neema, Amani na Uchumi.

Akitoa rai kwa wananchi mkoani humo, wakati wa kikao cha ushauri cha mkoa kilicholenga kujadili maandalizi ya dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mkuu wa mkoa wa Pwani alhaj Abubakar Kunenge alieleza, Rais Samia Suluhu Hassan imempendeza kushirikisha jamii ili kupata maoni na mawazo ya wananchi wenyewe.

“Rais angeweza kukaa na wataalamu na washauri wake mwenyewe lakini kwa hekima na utawala bora alionao,ametumia busara kutaka maoni ya kila mmoja,wakulima,wafugaji, taasisi binafsi,vijana, wanawake, viongozi wa dini,vyama wafanyabiashara, makundi maalum ili kuwa na muelekeo 2050”

Tunaweza tusiwepo sisi ambao tumetoa maoni yetu ila maoni haya yakafanyiwa kazi kwa faida ya vizazi vijavyo hata kama kutakuwa na mabadiliko ya kidunia ” alieleza Kunenge.

Vilevile Kunenge anampongeza Rais Samia kwa kutekeleza na kusimamia hali ya utekelezaji wa dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 .

“Tumeshuhudia Rais akisimamia yale yote yaliyoanzishwa na Serikali zilizopita na yeye kufanya makubwa nchini ilihali kuinua maendeleo na Uchumi ” alifafanua Kunenge.

Naye, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM Mkoani Pwani, Mwinshehe Mlao alieleza anahitaji Tanzania iendelee kuwa yenye amani, umoja na mshikamano.

Alisema,vitu hivyo ndio nyenzo ya kuinua maendeleo na Uchumi nchini. Mlao alitoa maoni yake ,anahitaji suala la umwagiliaji liwe kipaombele ili kupata chakula cha kutosha.

Alisisitiza,kuangalia kiini na chanzo kinachosababisha utovu wa nidhani kwa vijana na mambo yanayodidimiza maadili.

Nao viongozi wa dini, Sheikh Mkuu mkoa wa Pwani Hamis Mtupa, alisisitiza maadili mema na kusimamia elimu ya dini kuanzia kwenye familia.

Mtupa aliitaka serikali kuendelea kusimamia sekta ya utalii na miundombinu hasa ya barabara kwa kiwango cha lami.

Kadhalika alipenda kuona serikali ikiboresha miundombinu ya bandari Mafia kwa kuwa na gati ya uhakika na kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege.

Kwa upande wa vijana, Karimu Pazi aliomba serikali zijazo kutoa ajira bila upendeleo kwa vijana wenye vyeti mitaani kwani wapo vijana tangu wahitimu vyuo miaka 10 hawana ajira hivyo kupoteza muda na nguvu waliyotumia kupata elimu.

“Serikali inatumia nguvu kubwa kujenga miundombinu ya elimu,kuwekeza fedha ili kuona idadi kubwa ya watoto wanasoma hivyo ni vyema gharama zilizotumika zikazaa matunda kwa kuwapa ajira rasmi bila ukiritimba”

Pazi aliomba ,serikali kutoa mitaji na mikopo kwa vijana waliokosa ajira kutoka vyuo vya kilimo ikiwemo SUA ili waweze kujiajiri.

Mfugaji akizungumza kwa niaba ya wafugaji Ngobele Msamau alitaka kuona Tanzania inayomaliza migogoro ya wakulima na wafugaji.

Alisema, 2025-2050 wafugaji na wakulima watengewe maeneo yao na kujengewa miundombinu ili kuondoa migongano.

Kundi la wanawake akiwemo Asia Salum alitaka wanawake waongezewe mitaji na isiwe lazima kwenye makundi bali kwa mwanamke mmoja mmoja kulingana na ujasiriamali wa mtu binafsi.

Alitaka ,sheria zisimamiwe kwa wanawake na watoto wanaopata changamoto ya kunyanyaswa na kufanyiwa ukatili , na kuongeza kusiwe na upendeleo kwa wanaokutwa na tuhuma.

Asia alitaka , serikali isimamie katiba iliyopo lakini kubwa kuzingatia wachache wanaotaka katiba iwe inafanyiwa maboresho ili kuleta tija kwa watanzania.

Please follow and like us:
Pin Share