📌 Ni katika ziara ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan mkoani Tanga

📌 Vijiji vyote 118 vyafikishiwa umeme

📌 Naibu Waziri Kapinga ashiriki ziara.

Wananchi wa Wilaya ya Korogwe wameipongeza Serikali kwa utekelezaji wa miradi ya umeme Vijijini ambapo katika wilaya hiyo vijiji vyote vimefikishiwa umeme.

Pongezi hizo zimetolewa kupitia Mbunge wa Korogwe Vijijini Mhe. Timotheo Mzava leo Februari 24, 2024 wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Wilayani Korogwe kukagua miradi ya maendeleo.

“Tarehe 15 mwezi wa tatu 2021 ulikuwa kwenye viwanja hivi na sisi wabunge tulipata nafasi ya kusema.Tuliyoyaomba ikiwemo ya umeme vijijini umeyatekeleza tunakushukuru sana.” Amesema Mhe. Mzava

Amesema wakati huo wa ziara ya Rais Samia walieleza kuhusu changamoto ya upatikanaji umeme ambapo Vijiji 54 kati ya 118 vilikuwa havina umeme.

Mhe. Mzava ameongeza kuwa hivi sasa vijiji vyote 118 vya Korogwe Vijijini vimefikiwa na nishati ya umeme na wananchi wanaendelea kujishughulisha na shughuli za kiuchumi zinazotumia umeme.

Katika ziara hiyo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Naibu Waziri Nishati, Mhe. Judith Kapinga ameshiriki akimwakilisha Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko.