Rais Mstaafu wa Tanzania na Mjumbe Maalum wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete amefanya mazungumzo na Rais wa Niger, Mhe. Jenerali Abdourahamane Tchiani katika Ikulu ya Niamey April 16, 2025.
Katika mazungumzo hayo, Mhe. Kikwete ambaye ni mwanadiplomasia nguli aliwasilisha Ujumbe Maalum wa Rais Samia kwa Jenerali Tchiani.

Aidha, katika mazungumzo hayo, Mhe. Kikwete aliwasilisha salamu za Rais Samia ambapo alielezea kufurahishwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Niger na kusisitiza umuhimu wa kukuza na kuuimarisha zaidi katika nyanja za biashara, uwekezaji na utalii.
Alisisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kubadilishana uzoefu na ujuzi ili utajili mkubwa wa maliasili uliopo uweze kuvunwa na kuendelezwa kwa faida ya wananchi wa bara hilo.








