Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imepata tuzo ya ushindi wa utoaji wa huduma bora za afya kwa mwaka 2025 katika kundi la Hospitali maalum na Taifa.

Tuzo hiyo imetolewa leo na Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama wakati wa kufunga maadhimisho ya wiki ya Afya Kitaifa yaliyokuwa yakifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete kilichopo jijini Dodoma.

Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na mtoto Naima Kasiki aliyewahi kufanyiwa upasuaji wa moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maadhimisho ya wiki ya Afy

Akitoa tuzo hiyo Mhe. Jenista ameipongeza Taasisi hiyo kwa kuzingatia usafi wa maeneo ya kazi, utoaji wa huduma bingwa na bobezi, pamoja na utoaji wa huduma bora kwa wateja (customer care services).

“Taasisi hii imezingatia usafi wa mazingira na usalama kwa wagonjwa wanaowahudumia, nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnayoifanya”, alisema Mhe. Jenista

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema JKCI itaendelea kuboresha huduma inazozitoa huku ikiendelea kufikisha huduma hizo kwa wananchi waliopo mikoani kupitia kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimuelezea Waziri wa Afya huduma za utalii tiba zinazofanywa na Taasisi hiyo alipotembelea banda la JKCI wakati wa maadhimisho ya wiki ya Afya Kitaifa yaliyohitimishwa leo jijini Dodoma

“Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuendelea kuwekeza vifaa tiba vya kisasa katika Taasisi yetu na kuifanya taasisi hii kuwa kituo cha ubora Afrika Mashariki na kati katika kutoa huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo”, alisema Dkt. Kisenge.

Wananchi wa mkoa wa Dodoma wakipata elimu kuhusu magonjwa ya moyo kutoka kwa wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maadhimisho ya wiki ya Afya Kitaifa yaliyohitimishwa leo jijini Dodoma

Naye mkazi wa Dodoma Grace Ringo ameipongeza Taasisi hiyo kwa kutoa huduma bora kwa wagonjwa na kuokoa maisha ya watoto wanaohitaji matibabu ya moyo.

“Taasisi hii iliweza kuokoa maisha ya mtoto wangu aliyekuwa na matundu mawili kwenye moyo wake, walimfanyia upasuaji wa kuziba matundu hayo mwaka 2014 akiwa na miezi nane na sasa ana miaka 11 na afya yake ipo vizuri kabisa”, alisema Grace

Aidha Grace amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha Taasisi hiyo na kuweza kusaidi watoto kama ambavyo wakwake alisaidiwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na mtoto Naima Kasiki aliyewahi kufanyiwa upasuaji wa moyo akiwa na miezi nane katika Taasisi hiyo pamoja na pacha wake Neyman Kasiki (Kulia) walipotembelea banda la JKCI wakati wa maadhimisho ya wiki ya Afya Kitaifa leo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na baadhi ya viongozi wakati wa maadhimisho ya wiki ya Afya Kitaifa iliyomalizika leo jijini Dodoma