Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Mtwara

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe, amesema ujenzi wa Kongani ya Viwanda Maranje Newala mkoani Mtwara unalenga kuhakikisha ifikapo 2030, korosho zote zinabanguliwa nchini.

Amesema, lengo ni kuhakikisha wakulima hawauzi korosho ghafi nje ya nchi.

Bashe amesema hayo katika muendelezo wa ziara yake Mkoani Mtwara, wakati akizindua kiwanda cha kubangua Korosho cha TANECU kilichopo katika kijiji cha Mmovo, kata ya Kitangali Halmashauri ya Newala mkoani Mtwara.

Amesema, kiwanda hicho kilicho gharimu zaidi ya sh. Bilioni 3.4 kimelenga kufungua milango ya ujenzi wa mradi wa kongani ya viwanda Newala ambapo hadi kufikia mwaka 2030 korosho zote zitabanguliwa nchini.

Kiwanda hicho ni moja kati ya viwanda/Kongani kumi vitakavyojengwa katika eneo lenye mita za mraba 99,000.

Uwezo wa kiwanda kimoja ni kubangua tani 3,500 za korosho ghafi kwa mwaka.

Ametumia fursa hiyo kuutaka Ushirika nchini kubadili mfumo wake wa uendeshaji na kuzingatia mahitaji ya wakulima.

Waziri Bashe amesema anatambua kuwa taswira ya vyama vya ushirika nchini imebadilika kwani miaka michache iliyopita, vyama hivyo vilikuwa na madeni kila kona.

Pia, Bashe ameeleza mipango ya Serikali kufungua kiwanda kingine cha kuchakata tani 3,000 za Korosho Tandahimba ifikapo mwanzo wa Msimu wa mavuno 2025.

“Naomba kusisitiza kuwa, kabla ya mwisho wa mwaka huu,mizani ya kidigitali pia itakuwa imekamilika tayari kwa kuanza kazi,”amesema

Waziri Bashe ameeleza kuwa mpango wa serikali kuendelea kushirikiana na Bodi ya Korosho kuajiri maafisa ugani 400 mkoani humo ambao watashirikiana na vyama vya msingi vijijini kuandaa taarifa za wakulima na kusaidia kukua kwa sekta upo palepale.

Please follow and like us:
Pin Share