Mbunge wa Jimbo la Arusha mjini Mrisho Gambo,amemtaka Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya kaskazini Godbless Lema kuacha siasa za propaganda badala yake atumie fursa hiyo kuhamasisha wananchi kujiandikisha kwa wingi kwenye daftari la wapiga kura ili wapate haki yao ya msingi .

Gambo ameyasema hayo mkoani Arusha ,wakati akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa ufafanuzi juu maendeleo ya zoezi la uandikishwaji wapiga kura linaloendelea nchini kote.

Amesema kiongozi huyo wa Chadema anafanya siasa za kizamani na kueneza propaganda za uongo za kuharibu uchaguzi wa Serikali za mitaa.

Amesema kuwa Lema amekuwa akieneza propaganda za uongo kwamba Chama Cha Mapinduzi kinachukua majina ya wanachama Kutoka kwenye mitandao na kuwapa mawakala Ili wawaandikishe propaganda za uongo mtupu.

Amesema Chama Cha Mapinduzi kina misingi yake hivyo aache porojo zake asitunge maneno na kuaminisha umma .

“Hivi karibuni ametengeneza Propaganda moja ambayo tulimshtukia ya kukodisha Hiace Kutoka Njiro,na akawavalisha sare za shule Vijana na kuwapeleka Kituo cha kujiandikishia wapiga kura Cha Sakina ,aliposhtukiwa aliwaondoa lengo lake lilikuwa ni kuharibu zoezi la uandikishaji wapiga kura .”

Amesema ametafuta vijana amewapa magari mawili kwa ajili ya Propaganda za uongo lengo likiwa ni kukwamisha zoezi hilo ambapo magari anayoyatumia ni Toyota Rav 4, lenye Namba. T420;CAD na Spacio T 597 BMK kwa ajili ya kuvuruga zoezi hilo.

Amesema alikuwa amewaandaa vijana Ili wakavamie kwenye vituo vya kuandikisha wapiga kura ili ionekane hakuna amani hivyo anamtaka aache siasa za kizamani Rais Samia,ameleta miradi mingi ya maendeleo na wananchi wameliona hilo.

Katibu wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Amani Golugwa alipopigiwa simu kujibu hoja hizo za Mbunge Gambo kutuhumu kuwepo kwa magari mawili yanayotumika kuleta vurugu katika zoezi la uandikishaji amesema hakuna kitu kama hicho na kudai kuwa endapo Gambo ameona hayo anatakiwa kuyakamata kuyapeleka kituo cha Polisi ili sheria ichukue mkondo wake.

“Kwa kifupi tu niseme Gambo anatafuta atention ya kujibiwa na Lema lakini hawezi kumzungumzia maana hana madhara yoyote kwake , ameona Lema hamzungumzii popote hivyo anaamua kutafuta attention ili aanze kumzungumzia, na kuhusu hayo magari anayosema kama ana uhakika na ameyaona ayakamate apeleke Polisi ili sheria iweze kuzungumza, kwanini anazungumza na nyinyi waandishi na wakati Jeshi la polisi lipo kwa nini asiwaeleze” alihoji Golugwa.