Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amewaongoza Mawaziri wenzake; Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Jerry Silaa (Mb), katika kikao na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, anayesimamia nchi za Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Bi. Victoria Kwakwa , aliyepo nchini katika ziara ya kikazi, ambapo katika kikao hicho, Serikali na Benki ya Dunia, wamejadiliana masuala ya msingi ya kuendeleza ushirikiano kati ya pande hizo mbili ikiwemo uhifadhi na utalii pamoja na maendeleo ya watu na Taifa kwa ujumla.

Bi. Kwakwa alisifu na kupongeza ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Benki hiyo na kwamba Tanzania imekuwa nchi inayofanya vizuri kiuchumi kati ya nchi nyingi za Kusini mwa Jangwa la Sahara na ni mnufaika mkubwa wa programu mbalimbali zinazoendeshwa na Shirika hilo kubwa la Fedha duniani.