📌 Ni Eyasi-Wembere, Songo songo Magharibi na Mnazi Bay

📌 Jotoardhi nayo yatajwa Kongamano la Mafuta Afrika

📌 Kamishna Shirima atoa uhakika wa miundombinu ya gesi asilia Tanzania

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Dkt. James Mataragio amewakaribisha wawekezaji kuingia ubia na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa ajili ya utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini.

Dkt. Mataragio amewakaribisha wawekezaji wakati akitoa wasilisho la sekta ya mafuta na gesi Tanzani katika Kongamano la Wiki ya Mafuta (Afrika Oil Week 2024) lililofanyika Nchini Afrika Kusini, Tarehe 10 Oktoba 2024.

Amevitaja vitalu vya utafutaji wa mafuta na gesi asilia kuwa ni Mnazi Bay Kaskazini, Eyasi – Wembere, Songo Songo Magharibi, 41B na 41C na hii ni kutokana na taarifa zilizofanyiwa utafiti zinazoonesha viashiria vya uwepo wa rasimlimali hizo katika maeneo hayo.

Pia amekaribisha uwekezaji katika miradi ya kuzalisha umeme wa jotoardhi katika maeneo ya Ngozi, Kiejo-Mbaka, Songwe, Luhoi na Natron.

Dkt. Mataragio amesema Tanzania ni sehemu ya kuwekeza kutokana na utulivu wa kisiasa, mazingira rafiki ya uwekezaji, miundombinu wezeshi, uwepo wa soko la ndani na soko katika nchi jirani.

Vilevile, Dkt. Mataragio ameeleza jinsi Tanzania inavyotekeleza miradi mbalimbali mikubwa ya umeme ikiwemo mradi wa Julius Nyerere (JNHPP) ambayo inaiwezesha Tanzania kuwa na umeme wa kutosheleza mahitaji ya nchi na mwingine utauzwa katika nchi jirani.

Pia ameeleza kuhusu utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta la Afrika Mashariki (EACOP) ambapo Serikali ina hisa za asilimia 15 na mradi wa Gesi Asilia iliyosindikwa ( LNG) ambao majadiliano yake yanaendelea.

Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli na Gesi, Godluck Shirima wakati akishiriki katika mjadala wa kitaalam kuhusu uchumi wa gesi alieleza kuhusu miundombinu ya usafirishaji wa gesi iliyopo nchini ikiwa ni pamoja na bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam na mikakati ya Serikali ya kupeleka gesi katika nchi za jirani ikiwemo Kenya, Uganda na Malawi.

Aidha, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), Mha. Charles Sangweni alieleza kuhusu mpango wa Tanzania kutangaza duru ya tano ya vitalu 24 vya gesi asilia ambapo vitalu 21 vipo katika kina kirefu cha bahari ya hindi na vitalu 3 vipo katika ziwa Tanganyika.

Alieleza kuwa, vitalu vyote vina data za kutosha ambazo zinaashiria uwepo wa rasilimali za mafuta na gesi asilia hivyo aliwakaribisha wawekezaji katika mkondo wa juu kuchangamkia fursa hiyo.

Please follow and like us:
Pin Share