Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto M. Biteko, anatarajia kuwa mgeni rasmi katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme katika Mto Malagarasi wa megawati 49.5.

Kwa mujibu wa Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Nishati
Neema Chalila Mbuja amesema kuwa mradi huo utakuwa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa Kilovoti 132 kutoka Igamba hadi Kidahwe yenye urefu wa Kilomita 54 na Kituo cha kupoza na kusambaza umeme msongo wa kilovoti 400/220/132/33 cha Kidahwe mkoani Kigoma.

Amesema kuwa katika utekelezaji wa mradi wa Malagarasi, utagharimu jumla ya Dola za Marekani milioni 144.14 (sawa na shilingi za Tanzania bilioni 388) ambapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itagharamia kiasi cha dola za Marekani milioni 4.14 na benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB inagharamia kiasi cha dola za Marekani milioni140 kama mkopo wenye masharti nafuu.

Amesema kuwa mradi utahusisha sehemu kuu tatu ambapo sehemu ya kwanza itahusisha Ujenzi wa Bwawa la kuzalisha umeme ikiwemo tuta (Dam), njia za kupitisha maji (Waterways), jumba la mitambo ya kufua umeme (Powerhouse) lenye uwezo wa kuzalisha Megawati 49.5 pamoja na kituo cha kupokea umeme na kuuongezea nguvu wa msongo wa kilovoti 132 (Switchyard).

Amesema sehemu ya pili inahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa Msongo wa kilovoti 132 (Transmission Line) yenye urefu wa km 54 ambayo itaunganisha Kituo cha kuzalisha umeme na Gridi ya Taifa kupitia kituo cha kupoza umeme cha Kidahwe;

Ambapo amesema sehemu ya tatu inahusisha ujenzi wa mtandao wa usambazaji umeme katika vijiji saba (7) vinavyopitiwa na mradi ambavyo ni Mazungwe, Kidahwe, Mwamila, Kalenge, Kazuramimba, Mlela na Igamba.

“Mradi wa Malagarasi unatarajiwa kuzalisha umeme wa wastani wa Gigawati hour 181 kwa mwaka. Umeme huu utasaidia mahitaji ya ndani ya mkoa wa Kigoma, mikoa ya jirani pamoja na kuwezesha biashara ya umeme kikanda (Southern and Eastern Africa Power Pools), pamoja na kuboresha huduma za kijamii ikiwemo Elimu, Afya, maji pamoja na biashara za viwanda” amesema.

Please follow and like us:
Pin Share