Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Kenani Kihongosi, akiongea na Wanahabari mara baada ya hafla kumpokea rasmi mkandarasi, kampuni ya CCC (Beijing) Industrial & Commercial Ltd; kampuni kutoka China, tarehe 24 Oktoba, 2024, mkandarasi huyo ameanza rasmi kazi ya usambazaji umeme kwenye vitongoji 105 vya majimbo saba (7) ya mkoa wa huo.

……………….

Wateja 3,465 wataunganishwiwa huduma ya umeme

Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Simiyu

Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA); tarehe 24 Oktoba 2024 imemtambulisha rasmi mkandarasi; kampuni ya CCC (Beijing) Industrial & Commercial Ltd; kampuni kutoka China, itakayotekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme kwenye vitongoji 105 vya majimbo saba (7) ya mkoa wa Simiyu; Mradi utakaotekelezwa katika kipindi cha miaka miwili, kuanzia sasa.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Kenani Kihongosi, amempokea rasmi, mkandarasi, kampuni ya CCC (Beijing) Industrial and Commercial Ltd na kumuahidi ushirikiano wa kutosha ili atekeleze na kukamilisha Mradi kwa wakati.

Kihongosi amesema Mkoa wa Simiyu unamahitaji makubwa ya umeme kutokana na kuongezeka kwa viwanda vya vidogo na vya kati na kwamba hiyo ni fursa kwa Wananchi kukuza uchumi na maendeleo kwa ujumla.

Mwakilishi wa kampuni ya CICC (Beijing) Industrial and Commercial Ltd, Bi. Carol Wang (Aliyesimama) akitoa maelezo ya utekelezaji wa Mradi huo (Kulia na kushoto kwake) ni Watumishi wengine wa kampuni hiyo kwenye hafla hiyo.

“Namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa kipaumbele kwenye Sekta ya Nishati hususan umeme; nikitoa mfano kwenye usambazaji wa umeme kwenye vijiji, Simuyu vijiji vyote 470 vilishaunganishwa na huduma ya umeme na sasa tunapokea Mradi wenye thamani ya shilingi bilioni 15.6 na ambao Wananchi zaidi ya 3,465 watanufaika”. Amesema Mhe. Kihongosi.

Katika taarifa yake ya awali; Msimamizi wa Miradi ya REA mkoa wa Simiyu, Mhandisi, Deusdedit Msanze amemwambia Mkuu wa mkoa wa Simiyu kuwa, Wakala wa Nishati Vijiji (REA) umekamilisha Miradi ya kusambaza umeme katika Vijiji vyote 470 vya mkoa wa Simiyu kupitia miradi ya REA I, REA II, REA III Mzunguko wa I na I kwa nyakati tofauti.

“Mradi huu unalenga kufikisha umeme katika Vitongoji 105 vya Majimbo 7 ya Uchanguzi ya mkoa wa Simiyu ambapo kila Jimbo ni vitongoji 15. Mradi huu umeanza kutekelezwa tarehe 3 Septemba, 2024 na utakamilika tarehe 2 Septemba, 2026 Chini ya mkandarasi CCC (BEIJING) INDUSTRIAL & COMMERCIAL CO.LTD.”

“Mkandarasi huyo ataunganisha umeme kwenye Vitongoji 105 na kuunganisha Wateja 3465 ambapo vitongoji katika Majimbo hayo ni kama ifuatavyo; Bariadi (Vitongoji 15); Maswa Mashariki (Vitongoji 15); Maswa Magharibi (Vitongoji 15); Itilima (Vitongoji 15); Meatu (Vitongoji 15); na Kisesa (Vitongoji 15). Gharama ya mradi ni Shilingi 15,690,142,642.68 (pamoja na VAT).” Amekaririwa, Mhandisi, Msanze.

Msimamizi wa Miradi ya REA mkoa wa Simiyu, Mhandisi, Deusidedit Msanze akitoa taarifa ya utekelezaji wa Miradi mbalimbali katika mkoa wa huo mbela ya Mkuu wa mkoa huo wakati wa hafla hiyo, tarehe 24 Oktoba, 2024; kushoto kwake ni Katibu Tawala wa mkoa huo, Bi. Prisca Kayombo na kulia kwake ni Mhasibu Mwandamizi kutoka REA Makao makuu, Bi. Innocensia Makinge.

Kwa upande wake, Bi. Carol Wang kutoka kampuni ya CCC (Beijing) Industrial and Commercial Ltd; amesema kampuni yao, imejipanga ili kukamilisha Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 105 vya mkoa wa Simiyu kwa wakati na kuongeza kuwa sasa kazi inayoendelea ni ‘mobilization’ ya vifaa na Wafanyakazi ili kazi ya upimaji ianze.