Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia,

WAZIRI wa Kilimo Hussein Bashe ametoa saa 24 kwa kampuni ya RV inayonunua mazao Masasi mkoani Lindi kulipa madeni ya wakulima huku akiagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwashikilia viongozi wastaafu wa ushirika ambao wamehusika na ubadhilifu wa zaidi ya sh.milioni 139.

Pia amesema, serikali inakwenda kufumua mfumo wa mauzo na ugawaji wa ruzuku za pembejeo kwa kuwa hauna uwazi.

Akizungumza katika muendelezo wa ziara yake mkoani Mtwara Waziri Bashe ameelekeza kampuni ya RV ambayo ilishiriki mnada wa mbaazi kuhakikisha inalipa wakulima pesa ndani ya saa 24.

Walioshikiliwa ni pamoja Diwani wa Chiwale Yusuph Mataula aliyekuwa Katibu wa Amcos na Hashim Pahala aliyekuwa Mtendaji wa kijiji ambaye ameuza shamba hewa kwa mkulima.

Waziri Bashe alifikia uamuzi huo baada ya malalamiko ya wakulima ya kucheleweshewa malipo yao na kampuni hiyo.

Pia ameagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwashikilia waliokuwa watendaji wa vyama vya ushirika Hashim na Yusuph Mataula kutokana na tuhuma mbalimbali zaubadhirifu wa fedha za wakulima.

“Hawa kwa kuwa wamekiri, watatusaidia kujua wenzao waliotafuna fedha za wakulima ni lazima fedha hizi za wanyonge zirudi, haiwezekani mtu anapiga fedha katika ushirika anakimbilia katika udiwani,”amesema.

Waziri Bashe amesema, ili kufikia malengo ya mabadiliko sekta ta kilimo ni lazima kubadili mfumo wa mauzo na pembejeo.

“Kila aliyepewa nafasi hapa analalamikia mfumo wa mauzo na ugawaji wa pembejeo serikali tunakwenda kufumua hii mifumo ili iwe na tija kwa mkulima,”amesema.

Amesema mfumo wa mauzo sasa utahusisha wakulima kulipwa moja kwa moja na vyama vikuu huku mfumo wa ugawaji wa pembejeo ukihusisha maafisa ugani utakaoajiriwa ambao watahakiki wakulima na kugawa moja kwa moja badala ya pembejeo hizo kupewa viongozi.

Please follow and like us:
Pin Share