Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha
Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wakala wa Taifa wa Uhifadhi wa Chakula nchini (NFRA), Balozi John Ulanga amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini Rais Dkt Samia Suluhu Hassan umechangia mafanikio makubwa wakala kufanya mageuzi katika sekta kilimo.
Akizungumza Jijini hapa mara baada ya kumalizika kwa kikao cha Bodi ya Ushauri ya NFRA, Balozi Ulanga amesema Rais Samia kupitia Wizara ya Kilimo ameiwezesha Wakala kujenga uwezo wake ikiwemo kununua, kuhifadhi mazao kutoka kwa wakulima na kuuza katika masoko ya ndani na kimataifa.
“Uwezo wetu wa kuhifadhi mazao tunayoyanunua kutoka kwa wakulima umeongezeka sana kutoka tani takriba 250,000 miaka minne iliyopita hadi kufikia tani 776,000 yaani mara tatu zaidi,” amesema Balozi Ulanga.

Amesema Rais Samia kwa mamlaka yake aliwezakuridhia NFRA kukopa kwenye mabenki na kuweza kuongeza kiwango cha bajeti sambamba ile inayotolewa na Wizara ya Fedha.
“Kutokana na uungwaji mkono huo, tumeweza kununua zaidi ya tani 400,000 na kuwezesha wakulima kupata bei nzuri ya mazao yao na kubadilisha maisha yao,” alisema.
Kwa mujibu wa Balozi Ulanga, NFRA imeweza pia kujenga uwezo wa Kwenda masoko ya kimataifa na kuweza kuingia mikataba kadhaa mikubwa na mataifa na mashirika mbalimbali kama Zambia,Malawi, Congo DRC na Shirika la Chakula la Kuhifadhi Chakula Duniani(WFP).
Kwa upande wake,Mkurugenzi Mkuu wa NFRA, Dkt Andrew Komba amesema Wakala upo katika kufanya mageuzi makubwa ya kujenga uwezo wa kufanya biashara na kuhuwisha teknolojia.

“Kama Wakala tunajivunia mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka minne na mabadiliko mbalimbali tunayoendelea kuyafanya ili kufikia malengo na matarajio ya mheshimiwa Rais wetu,” alisema.
Sambamba na hilo, Dkt Komba amesema Menejimenti imepata wasaa wa kuwapitisha wajumbe wa Bodi ya Ushauri kwenye rasimu ya Mpango wake Mkakati wa miaka mitano wa 2026/27 mpaka 2030 ili waweze kutoa mchango wa mawazo yao na kuuboresha zaidi.
NFRA wameshawalipa wakulima kiasi cha shilingi bilioni 347 katika miezi minane iliyopita — kuanzia mwezi Julai 2024 hadi mwezi uliopita.


