Rais wa Rwanda Paul Kagame amezilaani nchi zinazoiwekea nchi yake vikwazo. Baadhi ya mataifa yameiwekea Kigali vikwazo kuhusu kuhusika kwake katika mzozo wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Akihutubia kwenye tukio la kuashiria mwanzo wa mfululizo wa shughuli za kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya 1994, Kagame amesema bila kuzitaja nchi zozote, kuwa zinapaswa kuyashughulikia matatizo yao na kumuwacha yeye akabiliane na ya kwake.

Waasi wa M23 wanaoungwa mkono na Rwanda wamekamata maeneo ya Kongo na kuikalia miji ya Goma na Bukavu. Watalaamu wa Umoja wa Mataifa wanakadiria kuwa Rwanda ina karibu askari 4,000 nchini Kongo wanaoliunga mkono kundi la M23.

Umoja wa Ulaya ulitangaza vikwazo dhidi ya makamanda watatu wa Rwanda, kufuatia uamuzi sawa na huo kutoka kwa Washington dhidi ya waziri mmoja wa serikali. Uingereza, Canada na Ujerumani pia zilisitisha baadhi ya misaada na na vibali vichache vya kuuza bidhaa nje ya nchi.