Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam
MAMLAKA ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imesema inatarajia kunadi vitalu 26 vya gesi asilia na mafuta kwa lengo la kuvutia wawekezaji ili kuchangia maendeleo na kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla.
Hayo yamebainishwa jijini Dar es Salaam Machi 5, 2025 na Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Mhandisi Charles Sangweni wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Kongamano la 11 na Maonesho ya Petroli nchi Wanachama Afrika Mashariki (EAPCE’25).

Sangweni amesema kuwa kati ya vitalu 26 vitakavyonadiwa, 23 vinapatikana katika Bahari ya Hindi, huku vitatu vikiwa katika Ziwa Tanganyika. Ameeleza kuwa kutokana na ugunduzi wa gesi katika maeneo hayo, kazi inaendelea ya kuzihakiki.
“Mpango wa Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuweka nguvu zaidi katika suala la utafutaji wa mafuta na gesi hasa katika kipindi hiki ambacho nchi inahamasisha nishati safi ya kupikia,” amesema Sangweni.
Amesisitiza kuwa mwaka huu kwao ni muhimu kwani kati ya shughuli wanazofanya ni kunadi na kuhamasisha uwekezaji katika tasnia ya utafutaji wa mafuta na gesi na kwa kuanzia PURA tayari wana maeneo hayo ambayo wameyawekea mipaka ili waweze kuwavutia wawekezaji kuja kuwekeza na kuanza shughuli hizo hapa nchini.
Aidha amesema kama watu wanavyofahamu Tanzania imegundua gesi kiasi cha futi za ujazo Trilioni 57.54 na kwamba gesi iliyogundulika kuna uhakika wa kupata soko hapa nchini na masoko ya nje kama Japan, Korea na nchi nyinginezo.
