Kesi iliyofunguliwa na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo dhidi ya Rwanda katika Mahakama ya Afrika ya haki za watu na zile za Binadamu inasikilizwa leo jijini Arusha – huku Kongo ikiishitaki Rwanda kwa kukiuka mipaka ya kimamlaka ya Kongo, kuchochea machafuko mashariki kwa Kongo na kusababisha uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu.
Kesi hiyo itakayosikilizwa kwa siku mbili Februari 12 na Februari 13 inahusu mapigano ya tangu Mwaka 2021, kati ya vikosi vya Kongo na waasi wa M23 ambao Kongo inadai wamekuwa wakifadhiliwa na Rwanda.
Kinshasa inadai kupitia mapigano haya Rwanda na washirika wake wamesababisha watu zaidi ya 500,000 kukimbia makazi yao, huduma za kijamii kama hospitali na shule kufungwa na hata kusababisha watoto zaidi ya 20,000 kukosa elimu.
Madai mengine ya Kongo dhidi ya Rwanda yanahusu kuhifadhi wahalifu wa kivita bila ya kuwachukilia hatua za kisheria au kuwarudisha Kongo ili waadhibiwe kisheria.
Kwa kuileta kesi hiyo katika Mahakama hiyo ya kikanda, Kongo inatumaini mahakama hii itaitia hatiani Rwanda kwa ukiukwaji wa Mamlaka ya Mipaka ya Kiutawala ya Kongo, kuchochea machafuko na kusababisha uvunjifu mkubwa haki za binadamu.
Kwa madai hayo, Kongo inataka Mahakama iamuru Rwanda kuacha kufadhili vikundi vya waasi, kuondoa wanajeshi wake katika mipaka ya Kongo na kulipa fidia kwa waathirika wa machafuko yaliyosababishwa .
Rwanda inakanusha madai haya, na hata kutiliashaka mamlaka ya mahakama hii kusikiliza kesi hii na inataka kesi itupiliwe mbali.
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/image-43.png)
![](https://www.jamhurimedia.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/ACHR-2.webp)