Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia Dar es Salaam

KAMPUNI ya kutengeneza magari ya Volkswagen ya Ujerumani imeonesha nia ya kuitumia Bandari ya Dar es Salaam kusafirisha magari na vipuri baada ya kuitembelea bandari hiyo na kueleza kuridhishwa kwake na ufanisi kufuatia uwekezaji na maboresho makubwa yaliyofanyika bandarini hapo.

Akiongea baada ya kutembelea eneo la kuhifadhia magari yanayowasili bandarini hapo kutoka nje ya nchi , Rais wa kampuni hiyo ya Volkswagen Martina Biene kwa nchi za Afrika ambaye pia ni Rais wa Chama cha Watengeneza magari Afrika (AAAM) amesema kuwa wameamua kuitembelea Bandari ya Dar es Salaam na kuangalia namna inavyofanya kazi na uwekezaji uliofanyika ili kuangalia namna ya kufanya kazi pamoja.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Bw. Plasduce Mbossa akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka jumuiya ya watengeza magari kutoka ujerumani waliokuja kujionea uwekezaji na maboresho yaliyofanyika katika badari ya Dar es salaam, akiwa na baadhi ya wafanyakazi wa TPA.

“Tumevutiwa sana na maboresho yaliyofanyika yakiwemo ya kimiundombinu ambayo yanavutia kuitumia bandari hii kwa ajili ya usafirishaji mizigo yakiwemo magari,”

“Na kupitia maboresho hayo, Bandari ya Dar es Salaam ina mchango mkubwa sana katika ukuaji wa uchumi katika bara la Afrika kwa sababu imekuwa ni kitovu cha biashara katika nchi nyingi katika bara hili,”

“Tukiwa kama wazalishaji wa magari na vipuri katika nchi mbalimbali duniani ikiwemo bara la Afrika, tunaiona Bandari hii ni kama kichocheo kikubwa cha biashara barani Afrika,” amesema.

Bienne, akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali waandamizi wa kampuni hiyo na kupokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) Bw.Plasduce Mbossa, alisema kuwa wamekuwa wakifanya pamoja na Serikali kupitia Wizara za Uchukuzi na ile ya Ujenzi na Miundombinu katika kuboresha sera na wamevutiwa na maboresho hayo.

Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es salaam Bw. Abed Gallus Abed akiwatembeza wageni kutoka jumuiya ya watengeza magari kutoka ujerumani waliokuja kujionea uwekezaji na maboresho yaliyofanyika katika badari ya Dar es salaam, akiwa na baadhi ya wafanyakazi wa TPA.

“Bandari ya Dar es Salaam ni eneo muhimu kwa ukuaji wa uchumi katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara na sisis kupitia kitengo chetu cha Afrika tunaona ni eneo muhimu la kibiashara,”amesema.

Akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA baaada ya ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa bandari ya Dar es Salaam Abeid Gallusi amesema kuwa jumuiya hiyo ya watengezjia magari kutoka Ujerumani illiamua kuitembelea Bandari hiyo kuona utayari wa kuitumia kwa ajili ya kupitisha magari na vipuri bandarini hapo.

“Wamevutiwa na utendaji kazi wa bandari yetu kwa sasa kupitia maboresho mbalimbali ikiwemo muda wa kuhudumia meli baada ya kuwasili bandarini kupungua kutoka siku 30 hadi ndani ya siku 7,”

“ Pia kupitia maboresho ya vifaa vya kisasa vya ulinzi na usalama, wizi wa vipuri vya magari yanayowasili bandarini hapa haupo kwa sasa na kuwapa wateja usalama wa mizigo yao yakiwemo magari hayo,”

“ Kwa kifupi wageni wetu wameridhika na tunategemea kufanya nao kazi pamoja,”amesema.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Bw. Plasduce Mbossa akimkabidi zawadi Rais wa Jumuiya ya Watengeneza Magari kutoka Ujerumani Bi. Martina Biene waliokuja kujionea uwekezaji na maboresho yaliyofanyika katika badari ya Dar es salaam.

Naye Arun George, Afisa wa Biashara wa DP waliowekeza bandarini hapo kutoka geti 0-7 amesema kuwa maboresho ya kimiundombinu yanaendelea katika idara mbalimbali ikiwemo ya kupakua mizigo ili kuleta ufanisi zaidi.

Amesema kuwa uwekezaji huu kwa kiasi kikubwa umerudisha imani kwa wafanyabiashara ambao hapo awali waliamua kutumia bandari za nchi jirani, lakini sasa hivi wanatumia tena bandari hiyo kupitisha aina mbalimbali ya mizigo ikiwemo madini aina ya Copper kwenda nchi za nje.

Kwa upande wa magari, amesema bandari hiyo inapokea magari 16,000 kwa mwezi, yakiwemo magari madogo, malori na mabasi kutoka nchi mbalimbali zaidi Japan na yanahudumiwa kwa muda mfupi sana ili kuwafikia wateja wakiwemo wanaoagiza kutoka nchi za mbalimbali za jirani ikiwemo Congo DRC, Zambia, Malawi na , Burundi.