Na Mwandishi Wetu (OR – TAMISEMI,) Simiyu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amechangia kiasi cha shilingi milioni 50, katika harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya msingi na umaliziaji wa majengo ya zahanati inayomilikiwa na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania – BAKWATA mkoa wa Simiyu.

Harambee hiyo iliyoendeshwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa – TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa imewezesha kukusanywa kwa shilingi milioni 150 ikiwa ni ongezeko la shilingi milioni 20 zaidi ya shilingi milioni 130  iliyolengwa.

Harambee hiyo imefanyika usiku wa Oktoba 12, 2024, katika adhimisho la Maulid ya Mkoa wa Simiyu kwa mwaka 2024, katika viwanja vya CCM wilayani Bariadi Mkoani Simiyu.

Akizungumza katika harambee hiyo Waziri Mchengerwa aliyepewa heshima ya kuwa mgeni rasmi katika adhimisho hilo la siku takatifu ya kuzaliwa kwa mtume, amesisitiza umuhimu wa elimu dunia na elimu ya dini kwa jamii, akisema elimu ndiyo silaha na nuru ya kujikomboa dhidi ya majanga yote anayokabiliana nayo mwanadamu Pamoja na kupata utukufu.

Kulikazia hilo Waziri Mchengerwa ameiomba BAKWATA iweke miongozo itakayo wajenga waumini katika kusimamia kikamilifu Uzalendo, maadili na kuipenda dini, watu na nchi yao, kuanzia ngazi ya awali, na kusisitiza jamii na wadau mbalimbali wausishwe, watoa mafunzo waanishwe na wajengewe uelewa na uwezo wa maarifa na mbinu kwa maeneo ya vijijini na mjini.

Alikadhalika Ameshauri kufanyika kwa mapitio yatakayokuja na maboresho ya mfumo wa uendeshaji wa elimu ya dini ya kiislam kwa marika yote makubwa na madogo ili kuweka ulinganifu wa mafunzo sahihi ya dini ya kiislam nchini.

“Utaratibu huo uguse kwa kina na upana, kijiografia katika maeneo ya vijijini na mjini hadi yasiyofikika kwa urahisi, uandaliwe mpango mahususi wa uwekezaji kwenye eneo hilo  ili kuimarisha miundombinu  ya madrasa na mifumo yake ya uendeshaji kwa kuimarisha vyanzo vya ndani vya rasiliamli za aina zote kwa kuwahusisha waumini ili kuweka utengamano sawia kati ya maeneo ya vijijini na mijini” alisema Waziri Mchengerwa. 

Katika Harambee hiyo Waziri Mchengerwa amechangia kiasi cha shilingi milioni 10, huku Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akichangia shilingi milioni 50 na kufanya lengo lililokusudiwa awali la kukusanya shilingi million 130 kuvukwa hadi shilingi milioni 150.

Awali Mufti mkuu wa Tanzania Sheikh Dkt. Abubakar Zuber miongoni mwa viongozi wakuu wa dini ya Kiislam walioshiriki katika Maulid hayo ameongoza dua ya kumshukuru na Kumwombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwataka waumini wote wa dini ya Kiislam kujitokeza kujiandikisha kwenye orodha ya wapiga kura wa serikali za mitaa, katika kipindi hiki ambacho Serikali inaendelea na zoezi hilo ili kuwapa sifa za kuwachagua viongozi wao katika uchaguzi wa serikali za mitaa Novemba 27, 2024.

Please follow and like us:
Pin Share