Katika Maonesho ya Madini Geita…

Mashine ya XRF ndio mpango mzima

HViongozi na wananchi wamiminika kupima madini yao

Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Gita

VIONGOZI na wananchi mbali mbali wameendelea kujitokeza kupata elimu kuhusu madini yaliyopo katika miamba na namna ya kupima sampuli za madini ya metali kwenye mashine ya XRF katika Banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya Saba ya Teknolojia na Uwekezaji kwenye Sekta ya Madini yanayoendelea kwenye viwanja vya Bombambili mkoani Geita.

Mashine hiyo ni maalum kwa kupima madini ya metali kwa njia ya mionzi /X-RAY na kisha kukupa majibu kwa kukuonyesha kiwango cha madini yote yaliyomo ndani ya metali hiyo kwa asilimia.

Akitoa elimu hiyo kwa viongozi na wananchi Afisa Maabara kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Edith Lewis amesema kuwa madini yapo ya aina nyingi duniani lakini huwa hayakai yenyewe, lazima yanakuwa yamechanganyikana na aina mbalimbali nyingine za madini katika miamba

Amesema, watu wanaonunua dhahabu ambao wanaogopa kutapeliwa kwa kuuziwa dhahabu feki wafike kwenye banda la Tume ya Madini kupata elimu ya namna ya kutambua miamba na madini mbalimbali pia wanaweza kupima hereni, mikufu ya dhahabu na shaba katika banda na kushauri wananchi kuitumia fursa hii kufika katika maabara ya Tume madini iliyopo Msasani- Tirdo Complex jijini Dar es Salaam ili kupima sampuli zao.

“Hii mashine ina kioo maalum itakuonyesha kwenye kioo madini yaliyomo ndani mfano ukipima dhahabu baada ya mionzi kuscan itakuonyesha dhahabu ipo asilimia 11 na Shaba ipo asilimia 89 sasa wewe ukiona hivi unajua moja kwa moja ulichouziwa ni feki ama si feki.

Amesema pia kuna mashine ya kupima sampuli za miamba kwa njia ya mionzi ambayo inatoa majibu ya ‘elements’ zote zilizomo kwenye huo mwamba na majina yake na wingi wake kwa kukuwekea asilimia yaani kama ni shaba utaona itaandika “Cu….%, kama ni madini ya chuma itaandika “Fe”….% kama ni dhahabu ipo itaandika “Au”….%.

Aidha, Mhandisi Edith ametoa wito kwa wananchi wanaofika kwenye maonesho ya Madini Geita kutembelea banda la Tume ya Madini ili pia kujionea vito mbali mbali na kujifunza fursa zilizopo katika sekta ya madini.

Kauli mbiu ya mwaka 2024 katika Maonesho ya Saba ya Teknolojia na Uwekezaji kwenye Sekta ya Madini ni Matumizi ya Teknolojia Sahihi na Nishati Safi katika Sekta ya Madini kwa Maendeleo Endelevu’.

Baadhi ya viongozi waliotembelea Banda la Tume ya Madini na kupata elimu ya upimaji sampuli ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Daniel Sillo, Mbunge wa Geita Mjini Constantine Kanyasu ambae pia ni mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini.

Viongozi wengine waliotembelea banda la Tume ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela, Kamishna wa Madini Dkt. Abdulrahman Mwanga, Mkurugenzi wa Blue Coast Ignas Inyasi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dkt. Venance Mwasse, Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbogwe, Dkt. Jacob Julius na Mwenyekiti wa UVCCM Geita Manjale Magambo.

Please follow and like us:
Pin Share