Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Pwani

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakari Kunenge amewahimiza wazee kuhakikisha kwamba wanaweka misingi mizuri na imara kwa ajili ya kuweza kumsapoti Rais wa awamu wa sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumlinda, kumtunza na kumtetea katika shughuli mbali mbali anazozifanya ikiwemo kuwatumikia wananchi wa Tanzania sambamba na kutekeleza miradi ya maendeleo katika sekta tofauti .

Kunenge aliyasema hayo wakati wa kilele cha maadhimisho wa siku ya wazee Duniani ambayo katika ngazi ya Wilaya yamefanyika katika Halmashauri ya Kibaha mji na kuhudhuliwa na wazee mbali mbali kutokana kata zote 14 za Kibaha mji pamoja na viongozi wa serikali, viongozi wa dini pamoja na viongozi wa vyama vya siasa.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Pwani alisema kwamba anatambua mchango mkubwa uliofanywa na wazee wa Mkoa wa Pwani hivyo ana imani wanaweza kumsemea mazuri Rais Samia kwa mambo mazuri ambayo ameyafanya kwa weledi mkubwa katika kuboresha sekta mbali mbali ikiwemo kuifanya Pwani kuwa na miradi mingi ya kimikakati ambayo itakuwa ni mkombozi mkubwa kwa wananchi.

“Mimi kama Mkuu wa Mkoa wa Pwani nimefarijika sana kukukutana katika siku hii muhimu ya maadhimisho ya wazee lakini kitu kikubwa ninachowaomba tumpe ushirikiano wa kutosha Rais wetu na kuhakikisha kwambaa tunamlinda na kumtetea kwa yale yote mazuri ambayo amekuwa akiyafanya katika nchi hii kwani ameweza kutenga fedha nyingi ambazo zimeweza kuleta matokeo chanya katika Mkoa wetu wa Pwani ikiwemo kuongoza kwa viwanda nchi nzima,” alisema Kunenge.

Kunenge pia alisema lengo la Serikali ni kuweka mikakati madhubuti ya kuendelea kuboresha huduma ya afya hususan kwa wazee ikiwa pamoja na kuwapatia vitambulisho maalumu ambayo vitaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika suala zima la kutambulika pindi wanapokwenda kupatiwa matibabu na huduma nyingine za msingi wanazostahili.

Kadhalika alifafanua kwamba wazee wa Mkoa wa Pwani wana busara nyingi hivyo wanapaswa kama wazazi na walezi kuweza kumpa amani na faraja Rais wao ili aweze kuendelea kuwatumikia wananchi wa Tanzania ikiwa pamoja na kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha huduma mbali mbali kwa wananchi na kuwaahidi kuwatembeza katika mirida ya kimikakati ili waweze kujionea na kujifunza mambo makubwa aliyoyafanya Rais Samia.

Kwa upande wake Mganga mkuu wa Halmashauri ya Kibaha mji Catherine Saguti amesema kuwa kwa sasa kuna jumla ya wazee wapatao 12,724 na kwamba wameweka mipango ya kuhakikisha wazee wote wanatambuliwa kwa lengo la kuweza kuwabaini ili kuweza kuwabaini na kuwapatia mahitaji yao ya msingi ikiwemo kuwapa kipaumbele zaidi katika mahitaji yao muhimu.

Dkt. Catherine aliongeza kwamba wanaendelea kutekeleza sera ya wazee ya mwaka 2003 ya kuwawezesha wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea kupatiwa fursa ya huduma ya matibabu pasipokuwa na vikwazo vyovyo vile hususan kwa wale wasiokuwa na uwezo wa kumudu ya kuchangia gharama mbali mbali za matibabu.

Pia alifafanua kwamba Halmashauri ya mji Kibaha katika kuwajali wazee hao imeendelea kutengeneza vitambulisho kwa ajili ya msamaha wa kuweza kupata matibabu bila malipo ambapo wameweza kuwafikia jumla ya wazee wapatao 8,540 ambao tayari wameshatengenezewa vitambulisho hivyo na kukabidhiwa.

Naye Afisa maendeleo ya jamii Halmashaauri ya Kibaha mji Rea Lwanji akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kibaha amebainisha kuwa siku ya wazee dunianiaa inalenga kuleta mabadiliko makubwa katika suala zima la uboreshaji wa maisha pamoja na kuwapatiaa huduma stahiki kwa ustawi wao wa siku za baadae.

Alisema kwamba serikali ya Wilaya ya Kibaha itakuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba inaboresha zaidi huduma kwa wazee wote na kwa kuzingatia utekelezaji wa sera ya mwaka 2003 ya kuwapatia wazee hao vitambulisho vya msamaha wa matibabu lengo ikiwa waweze kupatia huduma ya matibabu bila ya vigwazo vyovyote na kuwaweka katika mazingira ambayo ni rafiki katika maisha yao.

Nao baadhi ya wazee hao akiwwemo Rose Lwanda ambaye ni katibu wa Baraza la Wazee katika Halmashauri ya Kibaha mji ameishukuru Serikali japo bado wanakabiliwa na changamoto ya kutoingizwa kwenye mfumo wa Tasaf hivyo wameiomba serikali kuliangalia jambo hilo kwa jicho la tatu ili kuweza kuwasaidia waweze kupata fursa hiyo.

Kadhalika wameiomba Serikakali kupitia Halmashauri ya Kibaha mji kuwawekea mfumo mzuri wazee hao kuwaingia katika vikundi ili waweze kupata fursa ya kukopesheka kwa urahisi zaidi lengo ikiwa ni kuweza kujikwamua kiuchumi na kujiendeleza kimaisha ikiwa pamoja na kuomba kushirikishwa katika vikao mbali mbali vya kimaendeleo.

Please follow and like us:
Pin Share