Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

TANZANIA inatarajia kuwa nchi ya kwanza Afrika kuandaa uzinduzi wa mashindano ya Akili Mnemba na roboti ya vijana wa Afrika katika kongamano la nane la Tehama litakalowakutanisha wataalamu mbalimbali wa sekta hiyo kutoka nchi za Ulaya na Afrika.

Kongamano hilo linatarajiwa kufanyika Oktoba 13 hadi 17 mwaka huu, jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Jerry Silaa amesema kongamano hilo pia linalenga kubadilishana uzoefu kuhusu Tehama sambamba na kuhabarisha umma kuhusu mambo ya tehama ambayo yanafanyika nchini.

“Mkutano huu utaweleta wadau wote wa tehama duniani kuweza kubadilishana uzoefu, na kwa sasa dunia inazungumza kuhusu Akili Mnemba na imeanza kutumika nchini, ni kitu kigeni lakini kimeshika kasi, wizara itaendelea kuunga mkono Tume ya Tehama kuhakikisha malengo yake yanatimia,” Silaa amesema.

Mkurugenzi ya Tume ya Tehama Dk Nkundwe Mwasaga amesema kongomano hilo litajumuisha mada mbalimbali ambazo zitajadiliwa, ikiambatana na maonesho ya kampuni ndogo ndogo za Tehama yaani startup kwa vijana wa Tanzania.

Amesema tathimini ya mwezi wa tisa mambo ya usalama mitandao duniani iliyoifanya Tanzania kuwa katika rank ya kwanza duniani ni miongoni mwa sababu zilizoshawishi kufanyika kwa Kongamano hilo nchini.

Aidha amesema tathimini inaonesha kuwa Tanzania ipo katika nchi bora 25 duniani zinazotoa huduma za kidigitali, huku ikifanya vizuri katika mambo ya Startup.

Please follow and like us:
Pin Share