Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Malinyi


MKUU wa Wilaya ya Malinyi, Sebastian Waryuba amehamasisha wananchi kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa kukimbia mbio za kilomita tano.

Waryuba aliongoza wananchi na watumishi katika wilaya hiyo kwenye mbio hizo alizozipa jina la ‘Uchaguzi Marathoni 2024,’ ambapo Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unatarajiwa kufanyika tarehe 27 Oktoba 2024.

Mbio hizo zilianzia Mnarani kuelekea Kipingo Sekondari na kumalizia katika Viwanja vya Toboa tobo vilivyopo katika Kijiji cha Malinyi, Tarafa ya Malinyi wilayani humo.

Akizungunza na washiriki wa ‘Uchaguzi Marathon’ katika Viwanja vya Toboa tobo Waryuba alisema, ili kufikia lengo la uchaguzi wananchi wanapaswa kwanza kushirika zoezi la kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

“Malinyi Uchaguzi Marathon 2024 imelenga kuwahamasisha Wananchi wa Wilaya ya Malinyi kushiriki kikamilifu kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na baadaye kupig kura.

“Uandiskishaji katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utaanza tarehe 11 mpaka 20 Oktoba na kisha tarehe 27 Oktoba mwaka huu huu ndio itakuwa siku ya kupiga kura. Tujitokeze katika kujiandikisha,” Waryuba aliwaeleza wananchi.

Khamis Katimba, Mkurugenzi na Msimamizi wa Mkuu wa Uchaguzi katika Halmashauri ya Wilaya ya Malinyi alisema, watakaojiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kura ndio watakaopiga kura.

“Watumishi naomba tushirikiane katika kutoa hamsa kwa wananchi wajiandikishe katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

“Tukiwahamasisha vizuri watajitokeza. Wananchi wasipojiandikisha, watashindwa kupata haki yao ya msingi ya kushiriki uchaguzi na kuchagua viongozi wanaowataka,” alisema Katimba.

Kauli mbiu ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa mwaka huu, imeitwa “Serekali za Mitaa, Sauti ya Wananchi, Jitokeze kushiriki Uchaguzi.”

Please follow and like us:
Pin Share