Na Lookman Miraji, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Taifa la Saudi Arabia limeadhimisha miaka 94 tangu ilipopata uhuru wake kutoka mikononi mwa koloni la muingereza.

Kihistoria taifa la Saudi Arabia lilijipatia uhuru wake rasmi mnamo septemba 23 ya mwaka 1932 chini ya kiongozi wake mfalme Abdulaziz bin Abdul Rahman Al Saud ambaye anakumbukwa zaidi juu ya jitihada zake za kuwaunganisha raia wa taifa hilo na kuwa kitu kimoja.

Maadhimisho hayo ya 94 ya kitaifa ya Saudi Arabia yaliadhimishwa hapa nchini hapo jana septemba 23 na ubalozi wa Saudi Arabia nchini ukiongozwa na balozi wake Yahya bin Ahmed Okeish katika ukumbi wa hoteli ya kimaifa ya johari rotana dar es salaam.

Hafla ya sherehe hiyo ilijumuisha watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa kiserikali,mabalozi wa mataifa mbalimbali nchini pamoja na wanadiplomasia kutoka nyanja tofauti tofauti.

Mgeni rasmi katika shughuli hiyo alikuwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete ambapo aliwasilisha salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt: Samia Suluhu Hassan.

Kupitia hotuba yake Waziri Ridhiwani ameishukuru Serikali ya Saudi Arabia kwa ushirikiano wanauotoa kwa taifa la Tanzania kwani ushirikiano huo umelinufaisha taifa katika maeneo mbalimbali yakiwemi kilimo, elimu, ulinzi na usalama pamoja na huduma mbalimbali za kijamii.

Mafanikio katika sekta hizo yanaenda sambamba na ukumbusho na uhusiano thabiti uliopo baina ya Tanzania na serikali ya Saudi Arabia ambapo ziara ya mwisho iliyofanywa na madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo iliyofanyika chini ya mfalme Salman wa Saudi Arabia ni ushuhuda wa wazi kwani timu hiyo ya madaktari imefanikiwa kufanya upasuaji kwa watoto takribani 30 wenye matatizo ya moyo na kusaidia kuleta furaha na matumaini ya kuishi kwa watoto hao pamoja na familia zao.

Aidha pia Waziri Ridhiwani aliongeza kwa kutoa shukran za dhati kwa serikali ya Saudi Arabia kwa msaada mkubwa wanaoutoa katika miradi mbalimbali ya maendeleo kwa Serikali ya Tanzania na kuahidi kuwa Serikali na wananchi wataendelea kuthamini juu ya msaada huo usiokuwa na kikomo.

“Ningependa kutambua na kuishukuru serikali ya Saudi Arabia kwa msaada wake usioyumba katika miradi mbalimbali ya maendeleo ya serikali nchini Tanzania kupitia mfuko wa maendeleo wa Saudi Arabia (SFD). Serikali na wananchi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania wataendelea kuthamini na kushukuru kwa msaada usio na kikomo ambao umekuwa ukiotolewa kwa miaka mingi iliyopita katika sekta mbalimbali zikiwemo nishati, usafiri, maji na afya.” Aliongeza kwa kusema hayo waziri Ridhiwani Kikwete.

Kwa upande mwingine pia balozi wa Saudi Arabia nchini Yahya bin Ahmed Okeish nae kupitia hotuba yake ameahidi kuwa serikali ya Saudi Arabia itaendeleza uhusiano uliopo kati yao na Tanzania kwani bado wana nia na dhamira ya kudumisha uhusiano uliopo.

” Kupitia siku hii napenda kumhakikishia mheshimiwa kwamba ufalme wa Saudi Arabia unabadilishana ari na dhamira ya jamhuri ya muungano wa Tanzania katika kuimarisha uhusiano wake wa pande mbili katika nyanja mbalimbali kwa namna ambayo itafanikisha maslahi ya pamoja kwa nchi na watu wetu wawili marafiki, kwa kuzingatia urithi tajiri wa kitamaduni na mambo mengi ya kawaida hivyo tunatarajia kufikia upeo mpana”

Aidha pia balozi Yahya ameelezea utofauti wa taifa la Tanzania kwa kusema kuwa linatofautishwa sana na utulivu wa hali ya juu wa kisiasa na kiusalama unaojikita katika utamaduni wa kustahamiliana, kuelewana na ushirikiano miongoni mwa wanachama wa Tanzania.

“Mheshimiwa waziri jamhuri ya muungano wa Tanzania inatofautishwa sana na utulivu wa hali ya juu wa kisiasa na kiusalama unaojikita katika utamaduni wa kustahamiliana, kuelewana na ushirikiano miongoni mwa wanachama wake. Mbali na umuhimu mkubwa na unaokua wa kikanda wa nchi yako, Tanzania pia imeibuka kuwa nchi yenye nguvu ya kikanda kupitia juhudi zake na majukumu yake ya kupongezwa yenye lengo la kutuliza na kutatua tofauti na migogoro baina ya nchi za Afrika kwa njia za amani ambazo zimeimarisha nafasi yake ya kuwa nchi inayoongoza katika ukanda huo inayotaka kupata ustawi na ustawi wa watu wa Afrika” Aliongeza kwa kusema hayo balozi Yahya bin Ahmed.

Shughuli hizo zimefanyika mwaka huu wakati taifa la Saudi Arabia likiwa chini ya mtawala wake Mfalme Salman bin Abdulaziz Al Saud.

Please follow and like us:
Pin Share