Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameongoza hafla ya uwekaji jiwe la msingi kwa ujenzi wa maghala 28 mapya ya kuhifadhi nafaka katika eneo la Luhimba, Ruvuma.

Hafla hii imefanyika  Septemba 24, 2024, imekuja kama hatua muhimu kwa wakulima katika kuhakikisha uhifadhi bora wa mazao yao.

Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe (Mb), aliyehudhuria hafla hiyo, alieleza kuwa maghala hayo 28 ni sehemu ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wa maagizo ya Rais Samia ya kujenga maghala 70 vijijini, ambayo yana uwezo wa kuhifadhi jumla ya tani 28,000. Kila ghala lina uwezo wa kuhifadhi tani 1,000, jambo linalotarajiwa kuwa mkombozi mkubwa kwa wakulima wa maeneo husika.

Maghala hayo yatajengwa katika halmashauri nne za Wilaya, ambazo ni Songea Manispaa (ghala 1), Songea DC (maghala 11), Madaba (maghala 9), na Namtumbo (maghala 7). Waziri Bashe alibainisha kuwa tayari maghala matano kati ya 28 yameanza kutumika kuhudumia wakulima, huku mengine matano yakitarajiwa kukamilika katika wiki chache zijazo.

Ujenzi wa maghala haya unagharimu shilingi bilioni 14.7, ambapo kila ghala limejengwa kwa gharama ya shilingi milioni 527. Pia, Waziri Bashe alimueleza Rais Samia kuwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) ina mpango wa kujenga maghala makubwa ya kisasa yenye uwezo wa kuhifadhi tani 5,000 kila moja katika mikoa mitano yenye uzalishaji mkubwa wa mazao, ikiwa ni pamoja na Katavi, Rukwa, Ruvuma, Songwe, na Tabora.

Uwekezaji huu unalenga kuimarisha usalama wa chakula nchini na kutoa fursa zaidi kwa wakulima, huku ukionyesha juhudi za serikali katika kuhakikisha mazingira bora ya kuhifadhi mazao kwa maendeleo endelevu ya sekta ya kilimo.

Please follow and like us:
Pin Share