Na Dotto Kwilasa,JamhuriMedia,Dodoma

TUME huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini imetoa mwongozo wa maandalizi ya uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapigaji kura huku ikitoa nafasi kwa wafungwa na mahabusu kuandikishwa kuwa wapiga kura .

Hayo yameelezwa leo September 13,2024 jijini hapa na Mwalikishi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi Seleman Mtibora wakati akizungumza kwenye mkutano wa Tume hiyo na wadau wa Uchaguzi kuhusu uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura unaoendelea hapa nchini baada ya kuzinduliwa Kigoma Julai 20,2024.

Aidha ameeleza kuwa siku ya uzinduzi wa zoezi hilo ndiyo siku ambayo uboreshaji wa daftari ulianza katika mikoa ya Kigoma, Tabora, Geita,Kagera, Mwanza,Shinyanga, Mara, Simiyu na baadhi ya halmashauri za mkoa wa Manyara.

Amesema Tume hiyo imefikia uamuzi huo kutokana na kanuni ya 15(2)(C) ya kanuni za uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura za mwaka 2024 ambapo Tume imeweka utaratibu wa kuwezesha wafungwa magerezani /wanafunzi wa vyuo vya mafunzo Zanzibar na wanafunzi waliohukumiwa kifungo cha chini ya miezi sita kuandikishwa kuwa wapiga kura.

Mtibora ameeleza kuwa kwa Tanzania bara kuna vituo vya kuandikisha wapiga kura 130 vilivyopo kwenye magereza na kwa Zanzibar kuna vituo 10 vilivyopo kwenye vituo vya mafunzo (Magereza).

“Baada ya uboreshaji wa daftari kuanza, tumebaini kuwa wapo wapiga kura ambao mpaka sasa wana kadi zilizotolewa zamani zile karatasi za kabla ya mwaka 2015,wapiga kura hao watalazimika kwenda vituoni kuandikishwa upya kwa kuwa mfumo uliotumika wakati huo ni tofauti na wa sasa.

Sambamba na hayo ameeleza kuwa jumla ya wapiga kura 594,494 wanatarajiwa kuondolewa kwenye daftari la wapiga kura kwa kukosa sifa za kuendelea kuwepo kwenye daftari na kwamba baada ya uboreshaji inatarajiwa kuwa daftari litakuwa na jumla ya wapiga kura 34,746,639.

“Idadi hii inaweza kuongezeka kwa kuwa inawezekana wapo watanzania ambao walikuwa na sifa za kuandikishwa kuwa wapiga kura wakati wa uboreshaji wa daftari mwaka 2029/20 lakini kwa sababu moja au nyingine hawakuweza kujiandikisha kuwa wapiga kura, ” amesema

Kuhusu idadi ya wapiga kura wanaotarajiwa kupiga kura amesema, kwa kuzingatia matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 , jumla ya wapiga kura 5,586,433 wapya wanatajiwa kuandikishwa sawa na asilimia 18.7 ya wapiga kura 29,754699 waliopo kwenye daftari baada ya uboreshaji uliofanyika mwaka 2019/20.

Aidha idadi ya wapiga kura 4,369,531 inatarajiwa wataboresha taarifa zao ambapo kwa mkoa wa Dodoma Tume inatarajia kuandikisha wapiga kura wapya 450,005 idadi ambayo ni ongezeko la asilimia 34 ya wapiga kura 1,327,829 waliopo kwenye daftari la kudumu.

“Tume inatarajia baada ya uandikishaji mkoa wa Dodoma utakuwa na wapiga kura 1,777,834,katika maandalizi ya uboreshaji wa daftari tayari tume imekamilisha idadi ya vituo vya kuandikishia wapiga kura ambapo vituo 40,126 vya kuandikisha wapiga kura vitatumika katika katika uboreshaji wa daftari la mwaka huu, “ameeleza na kufafanua;

Vituo 39,709 vipo Tanzania bara na vituo 417 vipo Zanzibar ambapo ongezeko la vituo 2,312 ikilinganishwa na vituo 37,814 vilivyotumika 2019/2020, ” amesema Mtibora

Kwa upande wake Mkurugenzi msaidizi wa Daftari la TEHAMA Mbanga Rubibi ameeleza mfumo utakaotumika kuandikisha wapiga kura kuwa Tume itatumia vishikwambi vyenye mfumo wa Android badala ya kompyuta mpakato zilizotumika nyuma..

Amefafanua kuwa manadiliko hayo yamezingatia punguzo la uzito wa kifaa ambapo kwa sasa BVR itakuwa na uzito wa kilo 18 ikilinganishwa na ile iliyotumika katika uboreshaji wa 2019/20 ambayo ilikuwa na kilo 35 na kwamba manadiliko hayo yanalenga kurahisisha utiaji huduma.

Awali Mwenyekiti wa Tume huru ya Uchaguzi Jaji(R)(MST) Mbarouk S. Mbarouk ameeleza kuwa kwa mkoa wa Dodoma,mzunguko wa tano wa uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura utajumuisha halmashauri za Jiji la Dodoma, Bahi,Chamwino na Kongwa, Mkoa wa Manyara katika halmashauri ya Mji wa Mbulu, Wilaya ya Kiteto,Simanjiro na Singida.

Akiwasilisha taarifa yake Jaji Mbarouk amafafanua kuwa uboreshaji huo utaanza September 25,2024 hadi Oktoba 1,2024 na kwamba vituo vitakuwa vinafunguliwa kuanzia saa 2:00 asubuhi nankufungwa saa 12:00 jioni.

“Katika kuhakikisha kwamba Tume imaendana na manadiliko ya teknolojia ili kurahisisha zoezi hilo imeboresha mfumo wa uandikishaji ambao kwa mara ya kwanza utaenda kumwezesha mpiga kura kuboresha taarifa zake au kuhama kituo kwa kutumia aina zote za simu na kompyuta, ‘amesema na kufafanua kuwa;

Kwa wanaotumia simu za kawaida maarufu kama viswaswadu nao wanaweza kutumia huduma hii kwa kupiga namba 15200#na kisha watabonyeza namba 9 halafu wataendelea na hatua zingine kama itakavyokuwa inaelelezwa kwenye simu husika, “amefafanua

Kuhusu utaratibu wa watu wenye mahitaji maalumu, Mwenyekiti huyo ameeleza kuwa Tume imeweka Utaratibu kwa watu wenye ulemavu, wazee, wagonjwa, wajawazito na wakina mama wenye watoto wachanga watakaokwenda vituoni kupewa fursa ya kuhudumiwa bila kupanga foleni.

Pamoja na hayo amewatahadharisha wanaopanga kujiandikisha zaidi ya mara moja kuwa ni kosa kisheria kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 114(1) cha sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na madiwani Na. 1 ya mwaka 2024.

“Kifungu hichi kinasema mtu yeyote atakayeomba kuandikishwa zaidi ya mara moja atakuwa ametenda kosa kisheria na akitiwa hatiani adhabu yake ni faini isiyooungua shilingi laki moja au kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua miezi sita na kisichozidi miaka miwili au vyote kwa pamoja, “amesisitiza.

Kutokana na hayo baadhi ya wadau wa Uchaguzi wameishauri Tume hiyo kuona namna ya kuwezesha wafungwa wenye mahitaji maalumu kushiriki kikamilifu kwenye Uchaguzi ikiwa ni pamoja na kuwezesha huduma ya lugha ya alama kwa wafungwa viziwi.

Maiko Salali ameeleza kuwa kuna baadhi ya wafungwa hawana usikivu wa kutosha hivyo ni jukumu la Tume ya Uchaguzi kuhakikisha wanatoa Masada kwa wafungwa ili kupata sifa za kujiandikisha na kupiga kura kwa uelewa wa viongozi wanaowataka.

Please follow and like us:
Pin Share