Na. Andrew Chale, JamhuriMesia, Zanzibar

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwan Kikwete ambaye alikuwa mgeni rasmi ameweza kunogesha Bonanza la NMB DAY katika Tamasha la Kizimkazi 2024, linaloendelea katika maeneo ya Makunduchi na Kizimkazi, Kusini Unguja, Zanzibar.

Ridhiwani Kikwete ameweza pia kushiriki kucheza mchezo wa bao la kete ambalo alichuana vikali na Mhe Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Ayoub Mohammed Mahmoud ambao mchezo ulitoka sare sambamba na kushuhudia michezo mingine iliyokuwa ikishindanishwa katika Bonanza hilo.

Ridhiwani Kikwete aliweza kabidhi vikombe kwa washindi wa bonanza hilo, lililohusisha michezo ya Karate, Bao la Kete, Karata, Kufua na Kukuna Nazi, pamoja na Kuvuta Kamba.

Mbele ya Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi. Ruth Zaipuna, Waziri Kikwete aliwakabidhi Kizimkazi Dimbani vikombe vya Bao la Kete, Kuvuta Kamba (wanaume) na Karata na Kufua na Kukuna nazi, huku Kizimkazi ikitwaa vikombe vya Kuvuta Kamba (wanawake) na Drafti.

Katika mchezo wa kufua nazi (wanaume) na kukuna nazi (wanawake), Kassim Khamis Omar na Rukia Ibrahim wa Dimbani waliibuka washindi wakifuatiwa na Mosi Mtwana na Mwandari Khamis wa Mkunguni, huku Haji Hassan na Nasra Juma wa Mkunguni wakitwaa nafasi ya tatu.

Akifunga bonanza hilo, Waziri Kikwete aliwapongeza washiriki wote bila kujali matokeo yao, huku akiwataka kutumia vema fursa zilizoambatana na bonanza hilo, ikiwemo ya elimu ya fedha na kuwasisitiza kwamba wanapaswa kujenga utamaduni chanya wa kujiwekea akiba.

“Licha ya kuwapongeza kwa ushiriki na matokeo, wito wangu kwenu wakazi wa Kizimkazi Dimbani na Kizimkazi Mkunguni, nawasihi kutunza pesa zenu na NMB, msiweke fedha zenu vyumbani, mchagoni, fungueni akaunti hapa na muweke akiba na NMB,” alisema.

Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi. Zaipuna alimshukuru Waziri Kikwete kushiriki kukabidhi zawadi za washindi wa bonanza hilo, lililofuatiwa na Usiku wa Singeli, ambako wasanii wachanga na wakongwe wa aina hiyo ya muziki walipagawisha wananchi.

Licha ya kuzawadiwa vikombe, washindi wa NMB Day Michezo walizawadiwa fedha na kuingizwa katika akaunti zao walifungua wakati wa bonanza hilo, ambako huduma na elimu ya fedha, bima, mikopo na ufunguzi wa akaunti ulichangamkiwa na wakazi wa vijiji hivyo.

Please follow and like us:
Pin Share