*Maarifa ya asili ya Wahadzabe katika uhifadhi kuandikwa

Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Monduli

Taasisi ya wanahabari ya Usaidizi wa Jamii za Pembezoni (MAIPAC) imezindua mradi wa uhifadhi wa mazingira kwa kutumia maarifa ya asili huko Halmashauri ya Monduli na kuahidiwa kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kujifunza maarifa ya asili.

Mradi huo wa Mazingira unafadhiliwa na Mfuko wa Mazingira Duniani (GEF) kupitia program ya miradi midogo ambayo inasimamiwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa(UNDP) na kuratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira).

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Monduli Mkoa wa Arusha, Isack Joseph amezindua mradi huo leo, Julai 6,2024,katika hafla iliyofanyika Kigongoni mto wa mbu Wilaya ya Monduli.

Joseph akizungumza katika uzinduzi huo , amepongeza taasisi ya wanahabari wa MAIPAC kwa kubuni mradi huo. ambao unasaidia vita dhidi ya athari za mabadiliko ya Tabia nchi.

“Nawapongeza MAIPAC kwa kuja na mradi huu kwanza kujenga uzio katika chanzo cha maji cha Kabambe kata ya Selela lakini pia katika eneo la Eyasi kwenda kukusanya maarifa ya asili katika uhifadhi”amesema.

Mwenyekiti huyo, amesema halmashauri hiyo ipo tayari kutoa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kuhifadhi maarifa ya asili ambapo watu watakuja kujifunza Mila ,Tamaduni na maisha ya jamii za asili.

“Nimesikia maombi ya Mkurugenzi wa MAIPAC ,Mussa Juma kuomba ardhi kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha maarifa ya asili sisi tupo tayari kutoa ardhi tunaomba kuletewa barua rasmi ya maombi”amesema.

Awali Mkurugenzi wa MAIPAC ,Mussa Juma alisema mradi huo unatekelezwa kwa awamu ya pili awamu ya kwanza ilikuwa wilaya za Longido,Ngorongoro na Monduli na Sasa ni wilaya mbili za Karatu na Monduli .

Alisema lengo la mradi huo ni kusaidia uhifadhi wa mazingira,vyanzo vya maji na Misitu kwa faida ya sasa na vizazi vijavyo kwa maarifa ya asili.

“Tumebaini Kuna maarifa mengi ya asili ya uhifadhi mazingira hivyo MAIPAC tunakwenda kuyakusanya katika nakala ngumu na laini na baadae kutengeneza kitabu kwa awamu ya pili “alisema

Juma alishukuru GEF,UNDP na Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira kuendelea kutoa fedha kwa MAIPAC ili itekeleze miradi ya mazingira na kutunza vyanzo vya maji.

Alisema kwa mara kwanza MAIPAC inakwenda kukusanya maarifa ya asili ya jamii ya Wahadzabe na Datoga ili yaweze kuhifadhiwa na kutumika katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya Tabia nchi.

Akizungumza Kituo Cha Kutunza Maarifa ya asili alisema wanaomba kupatiwa ardhi ili kuanza mikakati ya ujenzi kituo ambacho pia kitakuwa kitega uchumi kwa jamii za pembezoni.

Awali Afisa wilaya ya Karatu, Reginald Hallu alisema wilaya hiyo kama wilaya nyingine zinakabiliwa na changamoto ya uharibifu na mazingira hasa kwa wananchi kulima katika vyanzo vya maji.

Hallu alisema halmashauri imekuwa ikichukuwa hatua mbalimbali Kudhibiti na akapongeza MAIPAC kuungana na serikali na kupeleka mradi wa mazingira lake Eyasi.

Naye Afisa misitu tarafa ya Manyara, Happy Masaki alisema mwaka juzi MAIPAC ilikuwa na mradi wa mazingira katika kata ya Selela na aliomba wajengewe uzio chanzo cha maji Kabambe na anashukuru MAIPAC kukubali na mwaka huu wanajenga.

Wakizungumza katika uzinduzi huo wananchi wa Selela na Eyasi walipongeza MAIPAC kuja na mradi huo na kuahidi wataendelea kutoa ushirikiano.

Halima Mollel mkazi wa Selela alisema wanaipongeza Taasisi ya wanahabari ya MAIPAC kurudi katika kata ya Selala kutekeleza mradi wa ujenzi wa uzio katika chanzo cha maji Kabambe..

Afisa miradi wa Shirika la Jumuiko la Maliasili Tanzania (TNRF) Stevin Ngowi na Mkurugenzi wa Shirika la MPDO ,Lebaraka Laizer ambao mashirika Yao yanafadhiliwa na UNDP pia walieleza MAIPAC limekuwa Shirika la mfano kwa kutekeleza vyama miradi.

Ngowi aliomba halmashauri ya Karatu na wananchi wa Eyasi kushirikiana vizuri na MAIPAC kama ilivyokuwa wilaya za Longido , Ngorongoro na Monduli .

Please follow and like us:
Pin Share