Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Kamati ya Uchaguzi ya Chama Cha Alliance For Democract Change (ADC) imepokea fomu za wagombea wa nafasi ya Uenyekiti Taifa na Makamu wake ili kujiandaa na mchakato wa uchaguzi ambao unatarajia kufanyika Juni 29, mwaka huu.

Wagombea hao ni aliyekuwa Katibu Mkuu wa ADC Taifa Doyo Hassan Doyo, ambaye anagombea nafasi ya Uenyekiti na Schola Kahana ambaye anagombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti.

Akipokea fomu hizo, Katibu wa Kamati ya Uchaguzi ADC, Innocent Siriwa amewataka wagombea wote kufuata taratibu na kanuni za uchaguzi ili Uchaguzi uwe wa amani.

“Hatua hii inaonyesha ukomavu wa kisiasa hasa pale ambapo viongozi wanapokubali kuachia madaraka kwa mujibu wa kanuni na sheria za katiba bila kulazimishwa.

“Natoa wito kwa wagombea kuzingatia taratibu zote zilizopo ili itakapofika tarehe 29, mwaka huu twende kwenye uchaguzi ambao tuna imani utakuwa huru na haki,” amesema Siriwa.

Akizungumza wakati akirejesha fomu hiyo, Doyo amesema ameona anatosha kugombea nafasi hiyo na endapo atafanikiwa atapambana Ili kuendelea kukiimarisha chama hicho kiweze kufikia viwango vya juu huku kikiwajali Watanzania katika masuala ya amani na utulivu.

“Kutokana na uzoefu wa miaka 10 nilioupata kutoka kwa Mwenyekiti aliiyemaliza muda wake naahiidi kuyaendeleza mazuri yote hususan kuilinda katiba ya chama chetu,” amesema Doyo.

Ameongeza kuwa, endapo atafanikiwa kushinda nafasi hiyo atakisaidia chama kusukuma ajenda za upatikanaji wa ajira, elimu bora, na kupata wabunge wawakilishi watakaowakilisha wananchi katika changamoto zao bungeni .

Please follow and like us:
Pin Share